Wednesday, August 1, 2012

HIVI UMEISIKIA KAULI YA GAZETI LA MWANAHALISI BAADA YA KUFUNGIWA NA SERIKALI? NDIO HII..

Siku moja baada ya Serikali kutangaza kulifungia kwa muda usiojulikana gazeti la kila wiki la MWANAHALISI linalochapishwa na kampuni ya Hali Halisi Publishers kutokana na kulituhumu kuandika habari za uchochezi na zinazoleta hofu, Uongozi wa gazeti hilo umezungumza.

Mkurugenzi mtendaji wa kampuni hiyo Said Kubenea amesema kimsingi hawakupokea barua rasmi kutoka Serikalini inayowataka kusitisha zoezi la kuchapisha gazeti hilo na badala yake hizo taarifa wamezipata kupitia vyombo mbalimbali vya habari.

Kubenea amesema hawakubaliani na madai ya serikali kwamba gazeti hilo limekua likiandika habari za uchochezi na kusisistiza kwamba habari yeyote inayoandikwa katika gazeti hilo ni lazima iwe imefanyiwa uchunguzi wa kina na kamwe gazeti hilo halikuwahi kukurupuka na kuandika habari isiyo ya kweli.

Inaaminika kwamba moja kati ya habari za hatari zilizofanya gazeti hilo kufungiwa kwa muda usiojulikana ni ile ya kuchapisha namba za simu za watu waliowasiliana na Dr Ulimboka mara ya mwisho kabla ya kufanyiwa ukatili.

Kwa kusisitiza, Kubenea amesema “hakuna kosa lolote tulilolifanya na tunastahili kupongezwa badala ya kulaumiwa, tulichofanya sisi ni kitu kidogo sana, tuliangalia tu ni nani aliwasiliana na Dr Ulimboka kwa mara ya mwisho… sasa tumepetaje? hizo ni taarifa zetu, kama kuna uchochezi ambao tumeufanya tulipaswa kuwepo Mahakamani lakini mpaka leo hatujaulizwa, hatujahojiwa, hatujaitwa hivyo ina maana hakuna kesi…. mimi kubenea nimefanya uchochezi ni kosa, naweza kufanya kosa kama hilo alafu natembea barabarani? “

No comments: