Wednesday, January 9, 2013

KIFO CHA MUMEWE... WASTARA SITASAHAU MAMBO HAYA MATANO

YAPO mambo mengi yanayomuumiza msanii wa filamu Bongo, Wastara Juma ambaye ni mke wa marehemu Juma Kilowoko ‘Sajuki’ lakini kuna matano ambayo mwenyewe anakiri hatayasahau.

Wastara aliyaanika mambo hayo hivi karibuni alipokuwa akizungumza na Risasi nyumbani kwake Tabata Bima jijini Dar.

Kutomnyoa ndevu
“Sajuki aliniomba nimnyoe ndevu alipokuwa amelazwa Muhimbili lakini sikufanikiwa kufanya hivyo. Nilikuwa nikitembea na mkasi kwenye pochi ila kila nilipokuwa nikitaka kufanya zoezi hilo, watu walikuwa wakija kumuona.”

Alimuomba asiondoke hospitalini
“Siku aliyoaga dunia jana yake aliniomba nisiondoke na kumuacha peke yake, kwa sababu zilizokuwa nje ya uwezo wangu niliondoka. Naumia kwa kuwa ningejua atakufa nisingeondoka.”

Ishu ya kumchezesha filamu
“Kingine kinachoniumiza ni kwamba Sajuki aliniomba turekodi muvi yetu ambayo ni mkasa wa mapenzi unaofanana na maisha yetu. Muvi hiyo tuliitunga miaka 2 iliyopita ambayo angecheza mpaka mauti yanamkuta, katika muvi hiyo aliomba acheze anakufa na kurudi tena. Nikikumbuka hili nazidi kuumia, sitasahau maishani mwangu.”

Gunia la mkaa lililokuja siku ya msiba
“Sajuki alikuwa akijua atakufa kwani siku ya X-Mas alikuja mjomba wake na kumuaga kuwa anakwenda Uganda. Akamuuliza Sajuki amletee zawadi gani, akamwambia amletee gunia la mkaa.
“Tuliokuwepo tulimshangaa na kumuuliza kwa nini? Akasema huo mkaa una kazi yake yeye amletee tu, cha kushangaza mjomba wake aliuleta siku ambayo ni ya msiba wake.”

Wimbo wa mwisho
“Cha mwisho kinachoniumiza ni wimbo wa mwisho wa marehemu ambao alikuwa akitaka nimrekodie kwa ajili ya Watanzania.
“Wimbo huo alisema utaitwa Nisameheni, cha kushangaza alipoanza kunishushia mistari akaanza kuchanganya na mambo yasiyoeleweka, nikahisi ameanza kuchanganyikiwa. Nilimuita daktari wake na hata lile zoezi la kurekodi halikufanyika tena.”

Kutoka: GLOBAL

Magazeti ya leo Jumatano 9th January 2013