Tuesday, July 31, 2012

Serikali Yahaha Kuzima Mgomo Wa Walimu

Mwanafunzi akipakizwa katika gari la Polisi baada kwenye kuvunjwa maandamano ya kuelekea kwa Mkuu wa Wilaya Kindononi kwa Wanafunzi kutoka shule za Msingi za Mtongani,Kunduchi,Mtakuja na Wazo kushinikiza walimu warudi kazini baada ya kusambaratishwa na Polisi katika eneo la Kunduchi jijini Dar es Salaam.Picha na Fidelis Felix


POLISI WAWATIA MBARONI VIONGOZI CWT, FFU WADHIBITI  WANAFUNZI DAR, TUCTA YAUNGA MKONO MGOMO

Waandishi Wetu
SERIKALI imelazimika kutumia Jeshi la Polisi katika harakati zake za kudhibiti mgomo wa walimu ambao jana uliingia katika siku yake ya pili, huku maandamano ya wanafunzi yakiendelea katika baadhi ya maeneo na Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU) kulazimika kuwadhibiti.

Taarifa kutoka mikoa kadhaa zinaonyesha kuwa polisi waliwakamata viongozi wa Chama cha Walimu Tanzania (CWT), ngazi za mikoa na wilaya, huku baadhi yao wakifikishwa mahakamani kwa tuhuma za kuchochea mgomo ambao Serikali tayari imesema kuwa ni haramu.

Kukamatwa kwa viongozi hao kulikwenda sambamba na tamko la baadhi ya wakuu wa mikoa na baadhi ya makamanda wa polisi ambao walionya kwamba wangewachukulia hatua za kisheria walimu ambao wangeendelea kugoma.

Wakati Serikali ikichukua hatua hiyo, Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (Tucta), limeitaka Serikali kuacha kujitetea katika suala hilo na kulipa madai ya wanataaluma hao wa sekta ya elimu.

Mkoani Dar es Salaam, FFU walitawanya maandamano ya wanafunzi katika eneo la Kunduchi, Kinondoni na kuwakamata baadhi yao. Waliandamana kwa madai ya kudai haki yao ya kufundishwa.
Kundi kubwa la wanafunzi waliodaiwa kwamba walikuwa wakitoka katika shule mbalimbali za Manispaa ya Kinondoni waliandamana katika maeneo ya Mbezi Machimbo, huku askari wa FFU wakijaribu kuwazuia na kuwaelekeza kurudi nyumbani.

Mmoja wa wanafunzi hao, Jamila Dadi alisema walimu wao wanaendelea kukusanya fedha za mafunzo ya ziada bila ya kuwafundisha, hivyo wameamua kuandamana ili kudai haki yao.

“Walimu wanakuja kila siku asubuhi wanachukua Sh200 kwa kila mwanafunzi, halafu wanaondoka bila kutufundisha ndiyo maana tumeamua kuandamana ili kudai haki yetu,” alisema Jamila.
Wanafunzi walioshiriki kwenye maandamano hayo wanatoka kwenye Shule za Msingi Wazo, Mtakuja, Mtongani, Kunduchi, Bwawani na Jangwani.

Wilayani Ilala, wanafunzi wa Shule ya Msingi Tabata walisababisha msongamano barabarani baada ya kuandamana kwa lengo la kwenda kwa Mkuu wa Mkoa ili awasaidie kuwarudisha walimu kazini ambao wapo kwenye mgomo.

Wanafunzi hao ambao walijikusanya asubuhi baada ya kufika shuleni hapo, walichukua uamuzi huo kutokana na kutosoma tangu juzi. Hata hivyo, waliishia Kituo cha Polisi cha Buguruni baada ya Mkuu wa Kituo, Inspekta Batseba  Kasanga kuwarejesha shuleni.

Mkoa wa Mbeya
Polisi mkoani Mbeya waliwakamata walimu wanne, Katibu wa CWT Wilaya ya Kyela, Petro Mangula (52) na Akso Kibona (52) ambaye ni Katibu wa chama hicho Wilaya ya Rungwe kwa tuhuma za kupita katika shule za msingi na sekondari kuhamasisha walimu waliokuwa wakiendelea na kazi washiriki mgomo.

Wengine waliokamatwa ni Mwalimu wa Shule ya Msingi Mbebe wilayani, Ileje Emmanuel Kyejo (45) na Mwalimu wa Shule ya Msingi Mkumbukwa, Anyangigwe Lwingwa (54).

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya, Athuman Diwani alisema kukamatwa kwa walimu hao kulitokana na taarifa za siri ambazo polisi walizipata kwamba walikuwa wakipita katika shule na kuwatishia walimu waliokuwa wakiendelea na kazi.

Diwani alisema watuhumiwa wote walifikishwa mahakamani jana katika mahakama za wilaya kujibu tuhuma zinazowakabili.

Alisema polisi pia inawashikilia watu tisa kwa tuhuma za  kufanya vurugu na kuvamia ofisi ya Mkurugenzi wa Mji mdogo wa Tunduma  na kuchoma nyaraka na  kupora mali mbalimbali  zenye thamani ya zaidi ya Sh117.515 milioni.

Vurugu hizo ni zile zilizotokea juzi saa 5.30 za asubuhi wakati wahalifu walipojichanganya katika maandamano ya wanafunzi waliokuwa wakipinga mgomo wa walimu.
Naye  Diwani wa Kata ya Tunduma, Frank Mwakajoka (Chadema) jana aliitisha mkutano wa hadhara ili kuzungumzia suala hilo na kulaani vikali vitendo vya uporaji  vilivyofanywa kwa mwamvuli wa maandamano ya wanafunzi.

Mwanza na Mara
Katika Mkoa wa Mwanza, Katibu wa CWT mkoani humo, Isaack Mashahushi alilalamika kwamba polisi wamekuwa wakiwakatama walimu kwa madai kwamba mgomo wao ni batili.
Mashahushi alisema wamepokea taarifa za kukamatwa kwa walimu watatu katika baadhi ya maeneo mkoani humo na kwamba ofisi yake ilikuwa ikiendelea kufanya mawasiliano zaidi ili kubaini kama wapo wengine waliokamatwa.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Liberatus Barlow alikataa kuzungumzia suala hilo, lakini akasema jeshi lake limejipanga kuhakikisha hakutokei vurugu.
Polisi Mkoa wa Kipolisi Tarime/Rorya wanamshikilia Mwalimu wa Shule ya Msingi Rebu, wilayani Tarime, Esther Kasika (40) kwa mahojiano baada ya kudaiwa kuhusika kuchochea watoto kufanya maandamano.

Kamanda wa Polisi katika mkoa huo, Justaus Kamugisha alisema mwalimu huyo anatuhumiwa kuwachochea wanafunzi wa Shule ya Msingi Rebu walioandamana juzi kwenda Ofisi Mkuu wa Wilaya Tarime kudai haki yao ya kusoma.
Kamugisha aliwataka walimu wote wanaotaka kufundisha kufanya kazi zao na endapo yeyote ataonekana kuwatishia, au kuharibu mali wanapaswa kutoa taarifa mara moja.

Tucta wang’aka
Katibu Mkuu wa Tucta, Nicholas Mgaya amesema Serikali inapaswa kutafuta ufumbuzi wa mgomo huo kwani unaathiri maendeleo ya wanafunzi.
Mgaya alisema Serikali haipaswi kujitetea katika suala hilo kwani walimu wana madai ya msingi ambayo yanatakiwa kufanyiwa kazi ili kuwawezesha kufanya kazi yao vizuri bila malalamiko ya mara kwa mara.

“Tunaitaka Serikali kulichukulia suala hili kwa uzito wa hali ya juu, kwani walimu wana madai ya msingi ambayo yanatakiwa kutekelezwa haraka. Kama haitakubali kulipa madai ya walimu, basi mgomo huo utawaathiri kwa kiasi kikubwa wanafunzi hasa darasa la saba na kwamba hata walimu hawatakuwa na moyo wa kufundisha vizuri,” alisema.

Mgaya alisema walimu wana haki ya kugoma na wanastahili kupewa haki zao kutokana na mazingira magumu wanayofanyia kazi, hasa ukizingatia hali ya maisha ilivyo wakati huu.

“Walimu wanafanya kazi katika mazingira magumu, sasa iweje wanapodai haki zao kwa lengo la kuboresha mazingira ya kazi mwajiri ambaye ni Serikali anajitetea kwa kutoa visingizio jambo ambalo haliwezi kukubalika. Tucta inaunga mkono mgomo huo kwa asilimia 100 kwani ni haki yao kufanya hivyo mpaka watakapopata stahili zao za msingi  wanazodai.”
Alisema mgomo huo ambao ulianza juzi umeathiri kwa kiasi kikubwa sekta ya elimu, jambo ambalo si jema kwa maendeleo ya nchi.

“Kwa siku moja tumeshuhudia mgomo huo ukiathiri sehemu mbalimbali za nchi sasa Serikali inapaswa kuliangalia hilo kwa kufikia makubaliano na walimu ikiwa ni pamoja na kulipa madai wanayoyataka,” alisema. SSoma zaidi; http://www.mwananchi.co.tz

Kubenea, Jukwaa La Wahariri Watoa Tamko Kuhusu MwanaHalisi Kufungiwa

Saed Kubenea - Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Hali Halisi inayochapisha gazeti la Mwana Halisi akionesha baadhi ya Magazeti yaliyolalamikiwa na Serikali

WAKATI Mkurugenzi Mtendaji wa Gazeti la MwanaHalisi, Saed Kubenea akiitaka Serikali kuondoa amri ya kulifungia gazeti lake, Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) limetoa tamko juu ya suala hilo.

Kubenea aliwaambia waandishi wa habari jana kwamba Sheria ya Magazeti ya mwaka 1976 ni katili kwa sababu haishauri Serikali kutoa maelezo ama kukumweleza mwenye gazeti juu ya nia ya kulifunga.
Kubenea alilazimika kuwaeleza waandishi juu ya suala hilo kufuatia kitendo cha Serikali kulifungia Gazeti la MwanaHalisi kwa kile ilichodai kuwa mwenendo wake wa kuandika habari na makala ni wa kichochezi, uhasama na uzushi.

Alisema yeye hakuitwa kujitetea , bali alipata barua kutoka Maelezo iliyokuwa na maelekezo ya kwamba amezuiwa kutoa gazeti na kwamba asome kwenye gazeti la Serikali namba 258 la Julai 27, mwaka huu. “Sheria hii katili ya magazeti ingali hai. Haijafutwa. Watawala wanaihitaji. Wanaitumia kutunyang’anya uhuru wa kufikiri, uhuru wa kutoa maoni na kuwasiliana, wamefanya hivyo kwa Mwanahalisi. Wametishia kufanya hivyo kwa vyombo vingine vya habari. Hii ni hatari,”alisema Mkurugenzi Mtendaji huyo.

Licha ya kuitaka Serikali kuondoa amri ya kulifungia gazeti lake, Kubenea pia aliwaomba wasomaji wao na wadau wengine wa habari kusimama nao katika kudai huru na haki ya kutafuta na kusambaza habari kwa sababu nchi hii ni yetu sote.

Katika hatua nyingine, Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), limelaani kitendo cha kufungiwa kwa Gazeti la Mwanahalisi, likitoa maelezo kuwa lengo la Serikali ni kuviziba midomo vyombo vya habari ili visifichue uovu unaofanywa katika mfumo wa utawala.

Taarifa ya jukwaa hilo ilisema kuwa, sheria ya magazeti ya mwaka 1976 ambayo Serikali imeitumia kulifungia gazeti hilo, ni moja ya sheria ambazo zimekuwa zikilalamikiwa na kuwa mara kadhaa yamekuwapo mapendekezo kwamba sheria hizo zifutwe.

“Uamuzi wa kulifungia MwanaHalisi haukubaliki na tunauona kama mwendelezo wa jitihada za Serikali kukandamiza uhuru wa habari na wanahabari nchini, lengo likiwa ni kuwaziba midomo wasiseme ukweli kuhusu uovu unaofanyika katika mfumo wetu wa utawala na jamii kwa ujumla,” ilisema sehemu ya taaifa ya TEF iliyosainiwa na Katibu Mkuu wake, Neville Meena.

Ilisema pia kuwa, uamuzi huu wa Serikali unaonekana una nia mbaya ndani yake, kwani adhabu ya kulifungia kwa muda usiojulikana ina tafsiri pana kwani inawezekana lengo la Serikali ni kulifuta gazeti la MwanaHalisi kijanja.

Naye wakili wa gazeti hilo, Legemeleza Nshala alisema Serikali ilikiuka ibara ya 18 kifungu cha 26 (1) na cha (2) na kifungu cha 30 (1) na cha 8 (2) (a)-(e) cha Katiba ya Jamhuri ya Muungano ya mwaka 1977. Alisema pia kuwa imekiuka Ibara ya 19 ya Agano la Kimataifa la Haki za Binadamu la mwaka 1966 na Ibara ya 6 ya Agano la Fungamano la Afrika Mashariki pamoja na Ibara ya 8 ya Agano la Haki za Binadamu na watu la Afrika la mwaka 1981.

Tamko La Chadema Kuhusu Kufungiwa Kwa Gazeti La Mwanahalisi


TAMKO LA CHAMA CHA DEMOKRASIA NA MAENDELEO (CHADEMA)

KUHUSU KUFUNGIWA KWA MWANAHALISI

Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kinalaani uamuzi wa Serikali inayoongozwa na Chama Cha Mapinduzi (CCM) kulifungia kwa muda usiojulikana gazeti la MwanaHalisi kwa kutumia mwanya wa sheria mbovu ya magazeti inayokwenda kinyume na haki za binadamu na utawala bora.

CHADEMA kinaitaka Serikali kulifungulia gazeti hilo haraka iwekanavyo na kimewasiliana na Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inayoongozwa na CHADEMA kuchukua hatua za kibunge kuisimamia Serikali kurekebisha udhaifu huo ikiwa inaheshimu uhuru wa habari na inazingatia maslahi ya taifa.

CHADEMA kinatafsiri hatua hiyo ya Serikali ya kufungia gazeti la MwanaHalisi kuwa ni sawa na kufungia uhuru wa kusambaza habari, uhuru wa kupokea habari na uhuru wa kutoa maoni, hivyo tunatoa mwito kwa wananchi na wadau wote wa habari kuungana pamoja kupinga hatua hiyo, na CHADEMA kitaeleza hatua za ziada za kuchukuliwa iwapo Serikali haitasikiliza kauli za wadau wa habari juu ya suala hili.

CHADEMA kinatambua kuwa uamuzi wa Serikali kufungia gazeti hilo kwa mara nyingine tena ni kwenda kinyume na haki za binadamu, kinyume na utawala bora na ni kikwazo kwa demokrasia na maendeleo nchini.

CHADEMA kinapinga hatua ya Serikali ambayo viongozi na watendaji wake wakiwa wametajwa kama watuhumiwa katika habari zilizoandikwa na gazeti hilo imetumia mamlaka haramu ya Waziri mwenye dhamana ya sekta ya habari kugeuka mlalamikaji, mwendesha mashtaka na mfungaji huku ikipuuza taasisi za kusimamia uwajibikaji na haki.

CHADEMA ilitarajia badala ya kulifungia gazeti la MwanaHalisi ingewezesha kufanyika kwa uchunguzi huru kufuatia habari za kiuchunguzi zilizoandikwa na gazeti hilo juu ya watendaji na watumishi wa Serikali kuhusishwa na jaribio la mauji ya Dr Ulimboka Steven, kupanga njama za mauji ya viongozi wa CHADEMA na matukio mengine ambayo yenyewe ndiyo yenye mwelekeo wa kufanya wananchi wapoteze imani na vyombo vya dola hali ambayo inaweza kuhatarisha amani na mshikamano uliopo nchini.

CHADEMA kinalinganisha uamuzi huo wa Serikali uliotangazwa tarehe 30 Julai 2012 na Msajili wa Magazeti chini ya Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo kuwa ni sawa kujichukulia sheria mikononi kwa kuwa Serikali yenye kuheshimu misingi ya asili ya haki ingezingatia kwamba ikiwa chombo chochote cha habari kimedaiwa kuvunja sheria ama kukiuka maadili dhidi ya Serikali, viongozi wake ama watu binafsi mashtaka au malalamiko yangepelekwa kwa taasisi zinazohusika mathalani Baraza la Habari (MCT) au mahakama.

CHADEMA kinafahamu kuwa Serikali imeamua kulifungia kutochapishwa kwa muda usiojulikana gazeti la MwanaHalisi, kwa mujibu wa Sheria ya Magazeti ya mwaka 1976, kifungu Na. (25) (i); hata hivyo uamuzi huo ni kinyume cha misingi ya asili ya utawala wa sheria.

CHADEMA kinaelewa kwamba zipo sheria nyingine katika nchi yetu ambazo Serikali ingeweza kuzitumia kushughulikia madai iliyoyatoa kuwa Gazeti la Mwanahalisi limeandika habari na makala za uchochezi, uhasama na uzushi kupitia mahakama lakini imeamua kwa makusudi kuendelea kutumia sheria mbaya isiyokuwa na uhalali wa kihaki (illegitimate).

CHADEMA kinakumbusha kuwa kwamba Sheria hiyo ni kati ya Sheria zilizotajwa na Tume ya kukusanya maoni juu ya mfumo wa vyama vingi (Tume ya Nyalali) kuwa ni sheria mbaya miaka 20 iliyopita kuwa na Sheria mbaya na Serikali imekuwa ikikwepa kutunga sheria mpya pamoja na wadau wa habari kuandaa miswada ya sheria ya huduma za vyombo vya habari na uhuru wa taarifa kwa nyakati mbalimbali.

CHADEMA kinatoa mwito kwa wananchi na taasisi zote za kitaifa na kimataifa kufuatilia kwa karibu tukio hili la kufungiwa kwa gazeti la MwanaHalisi na matukio mengine ya hivi karibuni kuhusu asasi za kiraia, makundi mbalimbali katika jamii ikiwemo madaktari na vyama vya siasa hususan CHADEMA yenye kuashiria kwamba Serikali inayoongozwa na CCM imeanza mkakati wa kuficha ukweli na kudhibiti mabadiliko kwa kutumia sheria kandamizi, vyombo vya dola na njia nyingine haramu.

Hivyo, ieleweke kwamba hatua hii dhidi ya Gazeti la MwanaHalisi ni mwanzo tu wa hatua zingine zaidi dhidi ya magazeti mengine na taasisi nyingine hali ambayo inahitaji wananchi na wadau wote kuunganisha nguvu za pamoja katika kuchukua hatua za haraka kuinusuru nchi na mwelekeo huo.

Imetolewa tarehe 30 Julai 2012 na:

John Mnyika (Mb)
Mkurugenzi wa Habari na Uenezi

Wabunge Wazidi Kuongezewa Marupurupu

MARUPURUPU ya wabunge ikiwamo mishahara imeongezwa kutoka Sh7.4 milioni kwa mwezi hadi takriban Sh11milioni kwa mwezi, hatua ambayo imeibua mjadala mwingine mzito miongoni mwao.

Tangu mwaka jana, wabunge wamekuwa katika vita ya kupokea au kutopokea posho ya vikao ambayo imekuwa ikikolezwa na Mbunge wa Kigoma Kaskazini (Chadema), Zitto Kabwe ambaye alizikataa akisema mbunge anapokuwa kazini hahitaji kulipwa.

Hata hivyo, uchunguzi wa gazeti hili umebaini kwamba sasa vita kubwa ipo katika marupurupu mapya ambayo pamoja na kuchanganya na mshahara yanafikia Sh11milioni kwa mwezi.

Spika wa Bunge, Anne Makinda alipoulizwa jana alithibitisha kuhusu kuongezeka kwa malipo jumla ya wabunge kwa mwezi lakini akasema hafahamu kiwango halisi kilichoongezwa.

Makinda alisema nyongeza iliyopo siyo kwa wabunge tu, bali watumishi wote wa Serikali na ilitangazwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (Menejimenti ya Utumishi wa Umma), wakati wa Bajeti ya Ofisi hiyo kwa mwaka 2012/13.

“Hiyo nyongeza siyo tu kwa wabunge, bali ni kwa watumishi wa Serikali. Tena hiyo ilitangazwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (Menejimenti ya Utumishi wa Umma). Sasa ukiniuliza kiasi gani hapo ndipo sielewei, ila najua nyongeza ipo,” alisema Spika.

Lakini, vyanzo kutoka ndani ya Bunge vilisema kwamba nyongeza hiyo ambayo tayari imeingia katika mshahara wa Julai ni Sh3.6milioni, hivyo kufanya jumla ya fedha anazochukua mbunge kufikia kiasi hicho cha Sh11milioni.
“Hiyo ni vita, kuna wabunge wana hasira kweli hawataki wananchi wajue kama marupurupu yameongezeka.

Wanaona wananchi wakijua itakuwa ni tatizo kubwa, watapigiwa kelele lakini nyongeza hiyo ipo. Tayari wengine wamechukua tangu Ijumaa,” kilisema chanzo kimoja kwa sharti la kutotajwa jina gazetini.

Hata hivyo, kwa mujibu wa chanzo hicho, baadhi ya wabunge kutoka kundi la wanaopinga posho kwa wabunge wamepinga pia nyongeza hiyo wakitaka fedha hizo zielekezwe katika sekta nyingine za kijamii.

Marupuru ya sasa
Hadi mwezi uliopita, mbunge alikuwa akipokea Sh7.4milioni kwa mwezi ambazo kati ya hizo Sh2.5milioni ni kwa ajili ya mafuta, Sh2.3 mshahara, Sh170,000 kwa ajili ya mshahara wa dereva, 100,000 kwa ajili ya katibu wa mbunge na posho ya jimbo.

Hata hivyo, katika nyongeza hiyo ya sasa haijawekwa wazi kwamba kiasi gani ni kwa ajili ya mshahara, fedha za mafuta ya gari la mbunge, za dereva, katibu na za posho ya jimbo na tayari baadhi ya wabunge wameanza kufuatilia mchanganuo wa nyongeza hiyo.

Chanzo:
http://www.mwananchi.co.tz/habari

Halmashauri Arusha angalieni usalama wa watu hawa!

 Baadhi ya wafanyabiashara wakiwa wamepanga bidhaa zao kando ya barabara na kuacha nafasi kidogo isiyoruusu magari kupishana, pia kujaza takataka nyingi katika mtar wa maji taka unaopita kando ya barabara hiyo.

Baadhi ya madereva wa Jijini Arusha wamelalamikia kitendo cha Halmashauri ya Jiji la Arusha kuruhusu shughuli za ufanyaji biashara kando kando ya barabara nje ya Soko Kuu la Arusha kwa kuwa mara kwa mara kumekua kukitokea kwa ajali na kusababisha hasa ya mali na maisha ya watu.

Madereva hao wasema kuwa wafanyabiashara hao wamekuwa wakigongwa na wengine kufa huku pia wateja nao wakigongwa na magari au pikipiki.

HASIRA ZA MKIZI FURAHA KWA MVUVI' NGASA SASA KUUZWA M 80

KLABU ya Azam Fc ya jijini Dar es Salaam, imetangaza katika ukurasa wake wa Facebook kumuuza mshambuliaji mahiri wa timu hiyo aliyejiunganao kwa dau kubwa akitokea Klabu ya Yanga, Mrisho Ngasa kwa dau la Dola za Kimarekani 50,000, ambazo ni sawa na Sh. milioni 80  za kitanzania.

Uongozi wa Klabu hiyo umeweka wazi kuwa umekasirishwa na kitendo cha mkali huyo kuonyesha mapenzi ya wazi kwa kuibusu Jezi ya Klabu yake ya zamani Yanga baada ya kuifungia timu yake bao lililoiwezesha kuipeleka timu hiyo hatua ya Fainali za Kombe la Kagame dhidi ya timu hiyo na AS Vita ya Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo, wakati akishangili bao lake mbele ya jukwaa la mashabiki wa Yanga.

Katika Mchezo huo Azam iliibuka na ushindi wa mabao 2-1 na kutinga hatua ya Fainali katika michuano hiyo, ambapo ilikutana na Yanga katika Fainali hizo mchezo uliochezwa mwishoni mwa wiki iliyopita katika Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam, ambapo Ngasa, aliingia akitokea benchi katika dakika za mwisho za mchezo huo.

Azam imeonyesha kukasirishwa na kitendo hicho cha Ngasa na kukielezea kuwa hakikua sahihi, ambapo awali uongozi huo ulikaliliwa kuwa ulikichukulia kitendo hicho kama tukio la kimichezo zaidi kutokana na mchezaji huyo kuwa alifanya hivyo huku akiwa tayari ametimiza majukumu yake ya uwanjani na kuwafungia bao muhimu katika mashindano hayo, na kuongeza kuwa hawakuona vibaya kwa Ngasa kuonyesha furaha yake kwa kushangilia kwa staili yake aipendayo.

Lakini sasa Uongozi huo umekuwa na kauli tofauti kuhusu tukio hilo ambapo sasa kama walivyojieleza katika mtandao wao wa Facebook, kuwa wamekasirishwa na kitendo hicho kilichoonyeshwa na Ngasa.

Aidha Uongozi huo umesema kuwa upo tayari kupokea ofa yeyote kutoka kwa timu yeyote iwe ya ndani ya nchi au nje ya nchi kwa dau hilo walilolitaja.

Uongozi huo ukionyesha hisia zake juu ya kukasirishwa huko, umeeleza kuwa mara kadhaa umemshuhudia Ngasa, akitinga katika Jengo la Klabu ya Yanga, kuwafuata rafiki zake Jerry Tegete, Hamis Kiiza na Niyonzima.
Mrisho Ngasa (kulia) akipozi kwa picha na Haruna Niyonzima, baada ya mchezo wa fainali za Kombe la Kagame uliozikutanisha timu zao jumamosi iliyopita, na Yanga kuibuka na ushindi wa mabao 2-0 na kutwaa Kombe la Kagame 2012 kwa mara ya pili mfululizo.

BALOZI WA PAPA NCHINI TANZANIA ATOA SAKRAMENT YA KIPAIMARA KWA MARA YA KWANZA KATIKA KANISA LA MT. PETRO OYSTERBAY

 Balozi wa baba Mtakatifu hapa nchini, Askofu Mkuu Fransisko Montecillo Padilla, akimpaka mafuta ya kipaimala Theodory Helon,  wakati wa ibada ya Sakaramenti ya kipaimara iliyofanyika katika kanisa la Mtakatifu Petro Osyterbay jijini Dar es Salaam jana. Jumla ya watoto 72 walipata sakramenti hiyo, kushoto ni mzazi wa kiroho  wa mtoto huyo, Daniel Mwisongo.
 Balozi wa baba Mtakatifu hapa nchini,  Askofu Mkuu Fransisko Montecillo Padilla, akimkabidhi Aivan Catrece, zawadi ya msalaba  wakati wa ibada ya Kipaimara iliyofanyika katika kanisa la mtakatifu Petro Osyterbay jijini Dar es Salaam.
 Baadhi ya watoto kati ya 72 waliopata sakaramenti ya kipaimara wakionyesha vyeti vyao baada ya kukabidhiwa na Balozi wa baba Mtakatifu hapa nchini Askofu Mkuu Fransisko  Padilla, wakati wa ibada hiyo iliyofanyika katika kanisa la Mtakatifu Petro Osytarabay jijini Dar es Salaam.
 Balozi wa baba Mtakatifu hapa nchini Askofu Mkuu Fransisko Montecillo Padilla, akikabidhiwa zawadi ya mbuzi na Catrece Theodory ambaye ni mmoja wa wajumbe wa kamati wakati wa Ibada ya kipaimara iliyofanyika jana katika kanisa la mtakatifu Petro oysterbay jijini Dar es Salaam.Kushoto ni Paroko wa parokia hiyo Joseph Mosha.
 Balozi wa baba Mtakatifu hapa nchini Askofu Mkuu Fransisko Montecillo Padilla, akiwahutubia watoto wa kipaimala  wakati wa ibada ya sakaramenti iliyofanyika katika kanisa la mtakatifu Petro Osyterbay jijini Dar es Salaam, Jumla ya watoto 72 walipata ekaristi hiyo.
 Balozi wa baba Mtakatifu hapa nchini Askofu Mkuu Fransisko Montecillo Padilla, akitoa baraka kwa waumini wa kanisa la Mtakatifu petro Oysterbay wakati wa Ibada ya Kipaimara,Askofu huyo ilikuwa mara yake ya kwanza kuongoza ibada katika kanisa hilo ambapo alisalimiana na waumini wote kwa kuwapa mikono na baraka.
Balozi wa baba Mtakatifu hapa nchini Askofu Mkuu Fransisko Montecillo Padilla, akitoa baraka kwa waumini wa kanisa la Mtakatifu petro Oysterbay wakati wa Ibada ya Kipaimara,Askofu huyo ilikuwa mara yake ya kwanza kuongoza ibada katika kanisa hilo ambapo alisalimiana na waumini wote kwa kuwapa mikono na baraka.
Mmoja wa watoto waliopta sakaramenti ya kipaimara katika kanisa la Mtakatifu Petro, Aivan Catrece, akionyesha kipaji chake cha kupiga ngoma wakati wa Ibada hiyo.

Kizaazaa Cha Mgomo Wa Walimu Manispaa Ya Singida...!

Wanafunzi wa shule ya msingi Ipembe, Nyerere, Unyankindi na Singidani ktk Manispaa Singida

Na: Elisante John Singida.
Julai 30,2012.

MGOMO Uliondaliwa na CWT nchini, umeleta madhara katika Manispaa Singida, baada ya wanafunzi wa shule za msingi kuandamana hadi ofisi ya RC leo.

Kwenye maandamano hayo, watoto wa shule ya msingi Nyerere, Singidani, Ipembe na Unyankindi, walitembea kilomita tatu hadi ofisi ya Mkuu Mkoa, huku barabarani wakiimba ‘tunataka haki zetu, walimu wamegoma, tunataka haki zetu’.

Baada ya askari polisi kubaini usalama wa watoto hao upo hatarini, waliingilia kati na kuongoza maandamano hayo hadi ofisi ya Mkuu wa Mkoa.

Wanafunzi hao zaidi ya 600 walijazana katika uwanja wa mbele, jengo la Mkuu wa Mkoa kuanzia saa tatu hadi saa 4:30 asubuhi.

Hatimaye Serikali ya Mkoa kupitia katibu wa tume idara ya Utumishi wa walimu Samweli Ole Saitabau, aliwataka kurudi nyumbani hadi kesho, wakaendelee na masomo katika shule zao.

Zitto Ahojiwa Kwa Rushwa

SAKATA la wabunge kuhusishwa na rushwa limeingia sura mpya, baada ya Naibu Kiongozi wa Upinzani Bungeni, Zitto Kabwe kuhojiwa na chama chake cha Chadema kwa saa tatu jana.
Wakati Zitto akihojiwa, kambi rasmi ya upinzani bungeni, iliwataja wabunge saba wa CCM na kueleza kuwa ndiyo wanaolichafua Bunge kwa kujihusisha na mambo yenye maslahi binafsi wakiwa watumishi wa umma.

Kadhalika, Naibu Spika wa Bunge, Job Ndugai alisema kwamba Taasisi ya Kuzuia na Kupamba na Rushwa (Takukuru) ilikuwa ikiendelea kuwahoji baadhi ya wabunge kuhusu tuhuma za rushwa na kwamba uchunguzi ukikamilika taarifa zitawekwa wazi.

Zitto ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Mashirika ya Umma (POAC) na Naibu Katibu Mkuu wa Chadema, jana aliandika katika ukurasa wake wa mtandao wa Tweeter kwamba alihojiwa na Sekretarieti ya chama chake kutokana na tuhuma za rushwa zinazowagusa badhi ya wabunge.
Katika maelezo yake, Zitto alisema aliiambia sekretarieti ya chama hicho kwamba Chadema kifanye uchunguzi ili kubaini ukweli wa suala hilo na kwamba yuko tayari kuwajibika ikiwa itathibitika kwamba alihusika kula rushwa.

“Kwa saa tatu nimejieleza mbele ya sekretariati ya chama kuhusu tuhuma za rushwa dhidi yangu. Niliomba kutaka kutoa maelezo kwa Katibu Mkuu, nimekiomba chama kufanya uchunguzi na ikibainika hatua zichukuliwe,” inasomeka sehemu ya taarifa hiyo kwenye Tweeter.

Lissu ataja wengine
Kwa upande wake, Mnadhimu Mkuu wa kambi hiyo, Tundu Lissu aliwataja wabunge wa CCM ambao wanatuhumiwa kuwa ni Nasir Abdallah (Korogwe Mjini), Mariam Kisangi (Viti Maalumu), Vicky Kamata (Viti Maalumu) na Charles Mwijage (Muleba Kaskazini) ambao hata hivyo, wote wamekanusha madai hayo.

Habari zaidi:  http://www.mwananchi.co.tz/habari

Gazeti La Mwanahalisi Lafungiwa

                                          JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
                              WIZARA YA HABARI, VIJANA, UTAMADUNI NA MICHEZO


                                                           TAMKO LA SERIKALI
                                         GAZETI LA MWANAHALISI LAFUNGIWA

Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imelifungia kutochapishwa gazeti la MwanaHalisi kuanzia 30 Julai, 2012 kwa muda usiojulikana kutokana na mwenendo wake wa kuandika habari na makala za uchochezi, uhasama na uzushi likiwa na nia ya kusababisha wananchi kukosa imani na vyombo vya dola hali inayoweza kuhatarisha amani na mshikamano uliopo nchini.

Katika matoleo yake hivi karibuni, gazeti la MwanaHalisi toleo Na. 302 la Jumatano Julai, 11 – 18, 2012 na toleo Na. 303 la Jumatano Julai 18 – 24, 2012 na toleo Na. 304 la Jumatano Julai 25 hadi 01 Agosti, 2012 na mengine yaliyotangulia yamekuwa yakichapisha habari na makala zenye kueneza na kujenga hofu kwa jamii.

Mhariri wa gazeti la MwanaHalisi, ameitwa na kuonywa mara nyingi, lakini hataki kukiri kuwa maudhui ya makala zake hazina tija kwa jamii, pia hazifuati weledi na maadili ya taaluma ya uandishi wa habari.
   
Mhariri, mara zote katika utetezi wake amekuwa akinukuu kifungu cha 18 cha Katiba ya nchi yetu ambacho kinatoa uhuru wa kutoa maoni na kwa makusudi kutonukuu kifungu cha 30 cha Katiba hiyo kinachoweka ukomo wa uhuru.

Uamuzi wa Serikali

Serikali imeamua kulifungia kutochapishwa kwa muda usiojulikana gazeti la MwanaHalisi, kwa mujibu wa Sheria ya Magazeti ya mwaka 1976, kifungu Na. (25) (i), adhabu hiyo itaanza tarehe 30 Julai, 2012 kwa mujibu wa Tangazo la Serikali (Government Notice) Na. 258 lililochapishwa katika Gazeti la Serikali na kutolewa jijini Dar Es Salaam tarehe 27 Julai, 2012

Serikali inawataka wamiliki, wahariri na wanahabari kuzingatia sheria, uzalendo, weledi na maadili ya taaluma ya uandishi wa habari katika kutekeleza wajibu wa kuhabarisha, kuelimisha na kutoa burudani kwa wananchi.

Kama ilivyoelezwa Bungeni wakati wa kuwasilisha Bajeti ya Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo hivi karibuni waandishi na watangazaji wa habari wanatakiwa kuhakikisha kuwa habari wanazoziandika na vipindi wanavyoandaa vinazingatia  taaluma na kuweka mbele maslahi ya Taifa letu na uzalendo. Uhuru na haki ya vyombo vya habari uendane na wajibu.

Kuanzia sasa Serikali haitasita kuchukua hatua dhidi ya vyombo vya habari ambavyo kwa maksudi vitatoa taarifa za uchochezi ambazo zitahatarisha hali ya amani na utulivu uliopo nchini mwetu.
Imetolewa na

OFISI YA MSAJILI WA MAGAZETI
WIZARA YA HABARI, VIJANA, UTAMADUNI NA MICHEZO
30 Julai, 2012

TAARIFA ZA MIKOA TOFAUTI KUHUSU MGOMO WA WALIMU PAMOJA NA KAULI YA WAZIRI.

Chama cha walimu Tanzania kimeanza mgomo wa walimu nchi nzima july 30 2012 ambao unatokana na walimu laki moja na elfu 53 kuukubali.

Ishu imekua nzito baada ya kushindwa kupata kile walichotaka kwa serikali ndani ya siku 30.

Wanachotaka ni kulipwa malimbikizo, ongezeko la mishahara kwa asilimia 100, posho za kufundishia kwa walimu wa sayansi asilimia 55 na walimu wa sanaa asilimia 50 na posho za mazingira magumu kwa asilimia 30.

Shinyanga walimu waliendelea na kufundisha kama kawaida, ambapo walimu wengi wakuu wamesema hawana taarifa zozote za kuanza kwa mgomo, yani hawakuambiwa chochote na bado wanaendelea na kazi.

Dar es salaam shule nyingi kumekua na mgomo mfano Mbezi Luis ambako wanafunzi walikwenda hadi kituo cha polisi Mbezi Luis kwa maandamano.

Kwenye mkoa wa Tanga shule kadhaa zimeonekana kuwa kimya huku wanafunzi wakiwa wenyewe shuleni, walimu wamegoma na wanafunzi kubaki kucheza tu na wengine wakarudi nyumbani.

Kwenye mkoa wa Pwani mgomo ulikuepo ambapo kwenye shule ya Mkoani wanafunzi walikua nje baada ya walimu kuondoka ambapo mwandishi wa habari Victor kasema kwenye shule ya Mtongani Mlandizi wilayani Kibaha ilikua kimya na imefahamika walimu waliwachapa wanafunzi walioingia darasani.

Amesema kwenye shule ya msingi Maili Moja mgomo ulikuepo ambapo baadhi ya wanafunzi walikua wakipiga mawe kwenye ofisi za walimu ambazo milango yake ilikua imefungwa, walimu hawajafanya chochote toka asubuhi.

Singida na Mbeya pia kumekuwepo na mgomo, kwa upande wa Mbeya kwa mujibu wa mbeyayetu Blog kuna vurugu kubwa ambayo mpaka Polisi waliingilia na kupiga mabomu ya machozi kutawanya wanafunzi walioandamana kushinikiza walimu wawape mitihani kabla ya kufunga shule.

Pamoja na hizo taarifa zote za mgomo, Waziri wa Elimu na mafunzo ya ufundi Dr Shukuru Kawambwa amesema mgomo huo ni batili lakini Serikali inawahakikishia walimu ambao hawajajihusisha na mgomo kwamba Serikali na vyombo vya usalama vitawalinda na kuwahakikishia usalama wao.

Amesema “tunawatahadharisha Walimu wote ambao wamegoma na wamekua wakiwatishia maisha walimu wengine ambao hawako kwenye mgomo, atakaebainika hatua za kisheria zitachukuliwa”

KAULI ZA BAADHI YA WABUNGE KUHUSU RUSHWA BUNGENI.

Baada ya kuwepo malalamiko ya rushwa kutembea bungeni na kusababisha kuvunjwa kwa kamati ya kudumu ya bunge ya Nishati na Madini mwishoni mwa wiki iliyopita, baadhi ya Wabunge wametaka majina ya wenzao wanaojihusisha na rushwa yawekwe wazi na wafukuzwe bungeni.

Mbunge wa Arumeru Mashariki Joshua Nassari (CHADEMA) amesema pamoja na kwamba kamati ya nishati na madini imetajwa moja kwa moja, zipo kamati nyingine ambazo wabunge wake wanatajwa kuhusika na kuomba rushwa.

Amesema “zipo kamati kadhaa zinatuhumiwa kwa rushwa, Mh Spika nilikua naomba muongozo wako kwamba kwa nini ofisi yako isiamue kuzivuruga kamati kadhaa ambazo zinatuhumiwa kwa rushwa ikiwemo kamati ya kudumu ya bunge ya Serikali za mitaa inayoongozwa na Mh. Mrema na Kamati ya kudumu ya bunge ya Mashirika ya Umma inayoongozwa na Mh. Zitto Kabwe, hii ni kwa sababu wabunge wengi wamekua wanazikimbilia zile kamati ambazo zina mikataba lakini kamati kama ya maendeleo ya jamii ya huduma za jamii ambazo zina umuhimu mkubwa kwenye nchi kwa sababu hazina mikataba zinakimbiwa”

Mbunge wa Lindi mjini Salum Khalfan na mbunge wa Nkasi kaskazini Ally keissy Mohamed wamelitaka bunge kuwafukuza bungeni wabunge wote watakaogundulika kula rushwa, wanataka watajwe kwa sababu sasa hivi wabunge wengine kila wakipita barabarani wanakosa raha kutokana na hiyo kashfa ya rushwa iliyolichafua bunge.

Baada ya hayo Naibu Spika wa bunge Job Ndugai aliomba kamati ya uongozi wenyeviti wa kamati za bunge kukutana na Spika kulizungumza ili baadae wampe maelekezo zaidi.