Thursday, August 30, 2012

TAARIFA KUTOKA SIMBA SC LEO

TIMU ya Simba inatarajia kucheza mechi dhidi ya timu ya soka ya NAIROBI CITY STARS siku ya Jumapili ijayo katika Uwanja wa Sheikh Amri Abeid Kaluta jijini Arusha.

Timu hiyo kutoka Kenya ndiyo iliyocheza na Simba jijini Dar es Salaam katika tamasha la Simba Day.

Awali Simba ilikuwa imepanga kucheza mjini Tanga WIKIENDI HII lakini kutokana na mabadiliko ya programu ya mazoezi ya benchi la Ufundi, Wekundu wa Msimbazi sasa watabaki Arusha hadi Septemba nne mwaka huu ili kukamilisha programu yote bila ya usumbufu.

Hali ya kikosi cha Simba ni ya utulivu kabisa na mazoezi yanafanyika kwa mchanganyiko wa mazoezi ya uwanjani na GYM.
Hakuna majeruhi yoyote hadi sasa na wachezaji wote wanafanya mazoezi kama kawaida.

Juma Kaseja
Kwenye mechi mbili za kirafiki zilizopita jijini Arusha, mlinda mlango namba moja wa Simba, Juma Kaseja, hakudaka na badala yake waliodaka ni Wilbert Mweta na Waziri Hamadi Mwinyiamani.

Kudaka kwa makipa hao ni mipango tu ya mwalimu na Kaseja hana maumivu yoyote na anafanya mazoezi kwa nguvu sana kujiandaa na msimu ujao.
Kama ilivyo ada, Kaseja atadaka siku ambayo mwalimu ataamua akae langoni

Felix Sunzu
Kuna baadhi ya vyombo vya habari vimeanza kuandika vichwa vya habari vyenye lengo la kuuza magazeti kutokana na kufiwa kwa mchezaji wetu huyu.
Simba SC inapenda kutumia nafasi hii kuviomba vyombo vya habari na wadau wengine kumuacha mchezaji huyu aomboleze msiba huu na siku yake ya kurudi itakapofika, klabu itatangaza.

Mussa Mudde
Simba SC inafahamu kiu ya vyombo vya habari kuhusiana na kutaka kujua masuala ya usajili wa wachezaji wake wa kigeni. Ukweli ni kwamba taarifa yoyote itakayotoka leo au kesho itakuwa haijaiva bado na klabu isingependa kutoa taarifa ambazo hazijaiva bado.

Tutatoa taarifa rasmi na kamili wakati mchakato mzima utakapokuwa umekamilika. Kwa hiyo, Simba haitatoa tamko lolote kwa sasa kuhusu usajili wa wachezaji wake wa kigeni hadi kila kitu kikamilike.

Tunaahidi kwamba hilo litafanyika haraka iwezekanavyo ili kiu yenu itimizwe.

Tunatanguliza shukrani
Imetolewa na
Ezekiel Kamwaga
Ofisa Habari
Simba SC
30/08/2012

Aina mbili za watu wanaoweza kukukatisha tamaa. Sema Hivi “Kama ninyi mmesoma na hamkufanikiwa, ni ninyi lakini mimi mafanikio yangu ni elimu.”

KWA sehemu kubwa, maisha ya mwanadamu yanategemea sana ushirikiano wa watu wenzake. Watalaamu wanasema mafanikio na kutofanikiwa ni watu.

Huwezi kusema umefanikiwa kisiwani kusikokuwa na watu ambao watakuwa sehemu ya mafanikio yako. Mtu yeyote hataonekana ameendelea kwa kuwa na viwanda vingi msituni wanakoishi wanyama wasiofahamu umuhimu wa nyama ya kusindika.

Aidha, kipimo cha kutofanikiwa hakitokani na maisha ya upweke bali ya kujilinganisha na watu wengine wanaozunguka maisha yako ya kila siku. Tajiri wa kijijini ni yule anayemiliki Bajaj ambazo wengine kwenye eneo analoishi hawana.

Ni ukweli ulio wazi kwamba utajiri wa mtu wa shamba wanakoishi maskini wengi hauwezi kuwanyima usingizi matajiri wa mjini wanaotembelea magari na kuishi kwenye nyumba za kifahari. Maana yangu hapa ni kwamba maisha ni watu.

Siku zote kwenye maisha yangu ninapokutana na binadamu wenzangu huwafikiria katika sehemu mbili. Kwanza kukwama kokote katika maisha kutatokana nao, lakini pili, ni  kufanikiwa kwangu sehemu ya ninachokitarajia kutoka kwao.

Ufahamu huu umenisadia sana. Kila mara niwapo na rafiki zangu huwatazama katika sura hizo mbili kwamba nifanikiwe au nisifanikiwe kwa ajili yao.

Nimetafakari na kuamini kuwa somo la aina mbili za watu wanaoweza kukukatisha tamaa kwenye maisha yako linaweza kukusaidia, msomaji wangu, kufikia ujuzi wa elimu ya jinsi ya kufahamu namna binadamu wenzako wanavyoweza kukuletea mafanikio au kutofanikiwa.

Bila shaka katika maisha yako umekutana na watu ambao walikukataza usifanye jambo fulani ambalo wewe uliamini kabisa lingekusaidia kufikia mafanikio uliyokusudia kwenye maisha yako.

Sikia kauli hii: “Jambo unalotaka kufanya haliwezi kufanikiwa, unajisumbua bure.” Yawezekana ulishaambiwa hivi na ukaogopa, ukasita, ukakata tamaa ya kuanzisha biashara kwa sababu rafiki, wazazi au ndugu zako wamekuambia hutaweza kufanikiwa.

Naomba ujifunze kwamba, watu ambao ni hodari kwa kauli za aina hii ni wale wanaotoka katika makundi mawili hatari. KWANZA ni wale wanaoogopa kujaribu kufanya jambo. PILI ni wale ambao hawapendi kukuona unafanikiwa kwenye maisha yako.

Mtu ambaye ni mwoga wa kujaribu,  usitegemee hata siku moja atakumbia “fanya”. Anachojua yeye ni kueneza woga wake. “Bwana usiende kubeba zege utapata matatizo ya kiafya, usifanye hiki na kile kuna hili na lile,” hizo ni baadhi ya kauli atakazokuambia.

 Hivyo, kuwa makini na watu waoga wa kujaribu, usiwape nafasi ya kukukatisha tamaa, hutafanikiwa kamwe!
Kundi la pili la kuwa nalo makini ni la wale ambao wanaogopa utafanikiwa. Watu ambao wanahofia uwezo wako utakufanya ufanikiwe na kuwashinda kwenye eneo hili na lile, watakupiga vita vya maneno ili kukukatisha tamaa, ubaki kama wao ambao hawakujaliwa uwezo ulio nao.

Puuza kauli za watu wasiopenda ufanikiwe, hata wakikuambia kuwa kusoma kwako hakutakusaidia waambie: “Kama ninyi mmesoma na hamkufanikiwa, ni ninyi lakini mimi mafanikio yangu ni elimu.” 

Asante kwa kunisoma.

Taarifa Kwa Umma Mauwaji Ya Morogoro

Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kinapinga kauli za Serikali, Jeshi la Polisi na Chama Cha Mapinduzi (CCM) zenye kulipotosha taifa kuhusu mashambulizi na mauji yanayoelezwa kufanywa na askari Mkoani Morogoro na badala yake kinataka uchunguzi huru ufanyike haraka kwa mujibu wa Sheria ya Uchunguzi wa Vifo (Inquest Act).

Kauli zilizotolewa na Waziri wa Mambo ya Ndani zina mwelekeo wa kulilinda Jeshi la Polisi ambalo askari na maofisa wake ni sehemu ya watuhumiwa wa mauaji, badala ya kuwezesha ukweli kuthibitika na hatua kuchukuliwa kwa wahusika.

Hivyokutokana na kujirudiarudia kwa mauaji yanayofanywa na vyombo vya dola CHADEMA kinatoa mwito kwa Rais Jakaya Kikwete ambaye kwa mujibu wa katiba ibara ya 33 ni mkuu wa nchi, kiongozi wa Serikali na Amiri Jeshi Mkuu aingilie na kuwezesha uchunguzi wa kina.

Ikumbukwe kwamba tarehe 27 Agosti 2012 Jeshi la Polisi Mkoani Morogoro lilifyatua risasi za moto na kupiga mabomu ya machozi wananchi na wanachama wa CHADEMA waliokuwa wamejikusanya kwa ajili ya kuelekea kwenye mkutano halali wa CHADEMA na wengine waliokuwa wakiendelea na shughuli zao eneo la Msamvu, hivyo kusababisha kifo cha raia mmoja asiye na hatia na kujeruhi wengine wawili.

CHADEMA kinaukumbusha umma kwamba kwa mauaji hayo na mengine katika maeneo mbalimbali nchini serikali inayoongozwa na CCM kupitia vyombo vya dola inaendelea kukiuka Ibara ya 14 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambayo inatambua kwamba uhai ni haki ya msingi kwa raia wote.

CHADEMA hakikubaliani na hatua zilizochukuliwa na Serikali mpaka sasa kuhusu tukio husika pamoja na maelezo yaliyotolewa na Waziri wa Mambo ya Ndani tarehe 28 Agosti 2012 ambayo kwa sehemu kubwa yametokana na taarifa zisizo za kweli kutoka kwa maofisa wa Jeshi la Polisi ambao ni sehemu ya watuhumiwa wa mauaji husika.

CHADEMA- Yapata Pigo Makete

Jumla ya vijana 47 waliokuwa wafuasi wa chama cha demokrasia na maendeleo (CHADEMA) katika kata ya Tandala wilayani Makete wamekihama chama hicho na kujiunga na chama cha mapinduzi (CCM) katika mkutano wa hadhara uliofanyika katani hapo

Mmoja wa vijana hao aliyejitambulisha kwa jina la Nahom Dovisiana Sanga amesema alijiunga na Chadema mwaka 2011 lakini ahadi alizoahidiwa ikiwa ni pamoja na kusaidiwa kiuchumi haijatekelezwa na ndio maana ameamua kutoka kwenye chama hicho

Naye Imani Nyamike ambaye ni mkazi wa kata hiyo naye amesema kwa upande wake amejiona kama amepotea kutokana na kukosa ushirikiano kwa viongozi wa chama hicho hivyo kujiona mpweke tangu alipojiunga na chama hicho

“Mimi napenda kuwaasa vijana wenzangu ambao mmmedanganyika na CHADEMA ndugu zangu huu ni muda wa kurudi CCM, bibi na babu yangu wapo CCM, baba na mama yangu wapo CCM na mimi nimerudi CCM na nitakufa ndani ya CCM” alisema Nyamike

Akizungumza mkutanoni hapo Katibu wa CCM wilaya ya Makete Miraji Mtaturu amesema chama chake kimefurahishwa na hatua iliyochukuliwa na vijana hao ya kujiunga na CCM na kusema wao kama chama cha mapinduzi wako tayari kuwasaidia vijana hao na kuwataka kujiunga na kuwa kikundi kimoja ili waweze kupatiwa mikopo ya riba nafuu ili wakuze mitaji ya bishara zao

Amesema kumekuwa na tabia ya baadhi ya vijana kujiunga na vyama vyenye sera za uongo pasipo kujua madhara yanayokuja kuwapata mbele na huku akisistiza wananchi waliofika kenye mkutano huo kubakia chama cha mapinduzi ambacho kimepewa dhamana na wananchi kutekeleza sera zake ndani ya wilaya hiyo

“Ndugu zangu naomba niseme CHADEMA hawana adabu, hivi hakuna ambayo jema lililofanywa na CCM hata mkapongeza? Ninyi kila siku ni matusi tu majukwaani, hata kitendo cha wao kuishi kwa uhuru hadi sasa ni jitihada za serikali ya CCM, bado nalo si jema kwenu?” alisema Mtaturu

Mtaturu alitoa bendera za CCM kwa vijana hao na kusema kuwa kwa kuwa tukio hilo la kuhamia CCM limetokea ghafla, atajipanga ndani ya chama chake kufanya sherehe ya kuwakabidhi rasmi kadi za CCM na kuongeza kuwa zoezi hilo litafanywa na uongozi wa mkoa ama taifa

Katika hatua nyingine Mtaturu aliwataka wananchi hao kuendelea kutoa ushirikiano kwa makarani wa sensa wanaoendelea na zoezi la kuhesabu watu katani humo kwani zoezi hilo bado linaendelea kwa siku saba mfululizo pamoja na wananchi hao kujiandaa kutoa maoni ya katiba mpya pindi tume ya kukusanya maoni itakapofika katani hapo

Naye diwani wa kata ya Tandala Mh. Egnatio Mtawa amewashukuru wananchi wa kata yake kwa ushirikiano wanaompa pamoja na kumuomba katibu wa CCm kusaidia kushughulikia suala la umeme wa gridi ya taifa kufika katani Tandala

Amesema huo ni mpango wa siku nyingi wa serikali kuhakikisha umeme unawaka Tandala hivyo anaombwa kusaidia kuimkumbusha serikali ili mpango huo ukamilike mapema

Chanzo: www.francisgodwin.blogspot.com

Rais Jakaya Mrisho Kikwete atuma Salamu Za Rambirambi Msiba Wa Askofu Kikoti

 
Baba Askofu William Pascal Kikoti.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete amemtumia Salamu za Rambirambi Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania, Mhashamu Baba Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa kufuatia kifo cha Askofu wa Kwanza wa Jimbo Katoliki la Mpanda, Baba Askofu William Pascal Kikoti.

Kifo cha Askofu Kikoti kilitokea jana Jumanne tarehe 28 Agosti, 2012 katika Hospitali ya Rufaa ya Bugando, Mkoani Mwanza alikokuwa amelazwa kwa matibabu kutokana na ugonjwa wa Shinikizo la Damu.

“Nimeshtushwa, nimesikitishwa na kuhuzunishwa sana kutokana na taarifa za kifo cha Baba Askofu William Pascal Kikoti wa Jimbo Katoliki la Mpanda akiwa bado na umri mdogo wa miaka 55 wakati ndiyo kwanza utumishi wake ulikuwa ukihitajika zaidi”, amesema Rais Kikwete katika Salamu zake na kuongeza,

“Ni dhahiri kwamba kifo cha Baba Askofu Kikoti kimeacha pengo kubwa la kiuongozi siyo tu kwa Kanisa Katoliki hapa nchini, bali pia Jumuiya ya Waamini wa Kanisa hilo kote duniani”.

Rais Kikwete amesema anatambua jitihada kubwa za Marehemu Baba Askofu William Pascal Kikoti enzi za uhai wake katika kuwatumikia Waumini wa Kanisa lake, na hususan wa Jimbo Katoliki la Mpanda, tangu alipopata Daraja la Upadre mwaka 1988, kuteuliwa kwake kuwa Askofu wa Kwanza wa Jimbo Katoliki la Mpanda mwaka 2000, na hatimaye alipowekwa Wakfu na Kusimikwa kuwa Askofu wa Jimbo hilo mwaka 2001.

“Kutokana na msiba huo mkubwa, ninakutumia wewe Baba Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania Salamu zangu za Rambirambi, na kupitia kwako kwa Kanisa Katoliki na kwa Waumini wote wa Kanisa hilo hapa nchini hususan wa Jimbo Katoliki la Mpanda, kwa kumpoteza mmoja wa Viongozi muhimu na wa ngazi ya juu wa kiroho, Marehemu Baba Askofu William Pascal Kikoti”, ameongeza kusema Rais Kikwete.

Amesema anamuomba Mwenyezi Mungu, Mwingi wa Rehema aipumzishe mahala pema peponi Roho ya Marehemu. Amewahakikishia wote waliofikwa na msiba huo kuwa yuko pamoja nao katika kipindi hiki kigumu cha maombolezo kwa kutambua kuwa yote ni mapenzi yake Mola.

Imetolewa na:
Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu.
Dar es Salaam.
29 Agosti, 2012

Pinda Akwepa Kumjadili Lowassa

WAZIRI Mkuu, Mizengo Pinda amekwepa kujibu tamko lililotolewa na  Waziri mkuu aliyejiuzulu, Edward Lowassa la kuupinga mpango wa Serikali wa kuboresha sekta ya kilimo kupitia mkakati wake wa Kilimo Kwanza.

Wakati Pinda akionyesha kutotaka kulizungumzia suala hilo kwa maelezo kuwa yupo kijijini,  Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika imepingana na maelezo ya Lowassa, kwa kueleza kuwa mpango huo umefanikiwa kwa kiasi kikubwa na kwamba waziri huyo aliyejiuzulu ana sababu zake binafsi.

Mwanzoni mwa wiki wakati akizungumza katika kipindi cha Dakika 45, kinachorushwa na Televisheni ya ITV, Lowassa alisema mkakati huo umekosa mashiko na kwamba kuna haja ya kubadili dhana yake na kuwa, elimu kwanza.
Alisema ni vyema ieleweke kuwa, Serikali inapaswa kutoa elimu kwa wananchi ili  waweze kuboresha mkakati wa kilimo kwanza.

Alisema pamoja na Serikali kuwa na nia nzuri ya kumkomboa mtanzania  kwa kuboresha mazingira ya kilimo, jambo hilo litakuwa si chochote kama mwananchi hatapatiwa elimu itakayomuongoza kwenye mapinduzi hayo ya kijani.

Akizungumza na Mwananchi jana, Waziri Pinda alisema, “Sijasikia kauli yake, siwezi kulizungumzia hilo kwa sababu sijui (concept) dhana nzima ya alichokisema.”

Hata alipoelezwa dhana ya alichokisema Lowassa Waziri Pinda alisema, “Kwanza nipo kijijini kwa kweli sijasikia na zaidi sijui kuhusu alichokizungumza.”

Wakati Pinda akieleza hayo Wizara ya Kilimo imepinga vikali, kauli ya Lowassa na kueleza kuwa mpango wa kilimo kwanza umefanikiwa kwa kiasi kikubwa, ndiyo maana hata idadi ya wakulima nchini imeongezeka.

Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Mohamed Muya alisema kuwa hivi sasa wakulima wanatumia dhana za kisasa za kilimo na kwamba hali hiyo imepunguza gharama ya kununua chakula kutoka nje ya nchi.

“Mpaka sasa tumepunguza gharama ya kununua chakula kutoka nje ya nchi, hii inatokana na wananchi kuongeza juhudi katika shughuli nzima za kilimo,” alisema Muya na kuongeza:

“Hiyo ni pamoja na kutumia zana za kisasa kwenye kazi hiyo, jambo ambalo limesaidia kuboresha mkakati wa kilimo kwanza.”

Alisema kuwa Lowassa anapingana na mpango huo kwa sababu zake binafsi, “ sijui kwanini anashindwa kukubaliana na ukweli kwamba, sekta ya kilimo imeimarika  tofauti na miaka iliyopita.”

Huku akitolea mfano kilimo cha mahindi alisema, kwa zaidi ya miaka mitano Serikali inazalisha zao hilo, kwamba hali hiyo inatokana na wakulima kupewa elimu ya kutosha juu ya kilimo cha mahindi na mbegu bora.

“Sasa hivi tumeweza kushirikiana na wadau mbalimbali kutoka ndani na nje ya nchi ili kuhakikisha kuwa, mpango huo unavuka malengo yaliyokusudiwa, ikiwa ni pamoja na kutoa elimu ya kutosha kwa wananchi juu ya kuboresha kilimo,” alisema Muya

Alisema Septemba mwaka huu, wanatarajia kufanya mkutano mkubwa wa sekta ya kilimo nchini, lengo likiwa ni kubadilishana uzoefu na wadau kutoka nchi mbalimbali.

“Jambo hili linaonyesha jinsi Serikali ilivyopiga hatua katika mpango mzima wa kilimo,” alisema Muya. CHANZO: MWANANCHI

Lowassa: Siungi Mkono Kilimo Kwanza

ASEMA HATA CCM INAJUA MSIMAMO WAKE.

Na: Peter Edson, Mwananchi.
WAKATI Serikali ikielekeza nguvu nyingi kutekeleza mkakati wa kuendeleza sekta ya kilimo nchini uliopewa jina la Kilimo Kwanza, aliyewahi kuwa Waziri Mkuu, Edward Lowassa ameibuka na kusema haungi mkono mkakati huo.Alisema mkakati huo wa Kilimo Kwanza umekosa mashiko hivyo ili auunge mkono, kuna haja ya kubadili dhana yake na kuwa, elimu kabla ya kilimo kwanza.

“Ni vyema nikaeleweka hapa. Ninachomaanisha ni kuongeza elimu katika Kilimo Kwanza ili wananchi wawe na elimu kwanza ndipo waweze kuboresha kilimo,” alisema Lowassa.

Akizungumza katika Kipindi cha Dakika 45 kilichorushwa na Kituo cha Televisheni cha ITV juzi usiku, Lowassa alisema pamoja na Serikali kuwa na nia nzuri ya kumkomboa mwananchi kwa kuboresha mazingira ya kilimo, jambo hilo litakuwa si chochote kama hatapatiwa elimu itakayomwongoza kwenye mapinduzi hayo ya kijani.

“Mpango huu wa Kilimo Kwanza umekosa nguvu kwa sababu kuanzishwa kwake hakukuzingatia dhana ya ukombozi wa mwananchi wa kawaida. Tangu awali ndani ya chama (CCM) nilieleza kuwa sitaunga mkono hoja hiyo mpaka kuongezwe mashiko na kuwa Elimu Kabla ya Kilimo Kwanza,” alisema Lowasa na kuongeza:

“Hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere alitoa uamuzi mgumu na wenye busara, ndiyo maana kilimo cha pamba, kahawa, mkonge na mazao mengine vikaanzishwa. Hivyo ipo haja ya kufanyika mchakato wa kuona mbali zaidi ili viongozi wetu waweze kutoa uamuzi sahihi katika hoja hii ya Kilimo Kwanza, kwani nguvu nyingi pasipo elimu inaweza kuligharimu taifa.”

Alisema kuwa ili mwananchi wa kawaida aweze kunufaika na Kilimo Kwanza, anahitaji kupatiwa elimu ya kutosha ya namna ya kuandaa mazingira ya kilimo na uelewa wa vifaa na pembejeo za kilimo ikiwemo mbolea na dawa.

Alisema pamoja na kuwa na mabwana shamba wachache, wananchi wamejikuta wakitumia mawazo yao kufanikisha miradi ya kilimo katika maeneo yao na matokeo yake wanapata mazao kidogo ambayo hayawakwamui kiuchumi.

Alitoa mfano wa nchi ya Indonesia akisema inaendesha uchumi wake kwa kilimo cha michikichi, ambayo mbegu zake zimetoka Tanzania... “Lakini Tanzania iliyotoa michikichi hiyo sasa ni moja ya wateja wa mafuta hayo yanayotoka Indonesia.”

Alishauri Serikali kuanzisha mashamba ya michikichi maeneo mbalimbali nchini kwa kuwa ardhi ipo ya kutosha hivyo kujitosheleza kwa mafuta hata ya kuuza nje.

“Ningelikuwa na uwezo wa kutoa uamuzi, vijana wetu wa JKT (Jeshi la Kujenga Taifa), ningewapa kazi ya kuanzisha mashamba ya michikichi nchi nzima kwani nchi yetu imejaliwa kuwa na ardhi kubwa na yenye rutuba, mapori yapo mengi,” alisema Lowassa.

Alisema wananchi wanaweza kupewa matrekta na pembejeo mbalimbali za kilimo, lakini bila kupewa elimu elekezi ya namna ya kuzitumia pembejeo hizo kuzalisha mazao bora, itakuwa kazi bure kwa kuwa ongezeko la mazao litakuwa dogo kama ilivyo kwa kilimo cha jembe la mkono.

Alitoa wito kwa Serikali kutumia fursa zilizopo za miradi ya kilimo kuwaelimisha Watanzania ili baadaye waweze kupewa au kukopeshwa zana za kilimo, akieleza kuwa nguvu kazi na elimu, ndivyo vitakavyomkomboa mwananchi katika umaskini wa kipato.

  Chanzo: http://www.mwananchi.co.tz

Magazeti ya Leo Alhamisi 30th August 2012


MATOKEO YA REAL MADRID VS BARCELONA NA WAFUNGAJI WAKE AUGUST 29 2012.