Thursday, August 2, 2012

HOTUBA YA MHE. DKT. JAKAYA MRISHO KIKWETE, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, KWA WANANCHI, TAREHE 31 JULAI, 2012

                                 HOTUBA YA MHE. DKT. JAKAYA MRISHO KIKWETE,
                                 RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA,

Ndugu Wananchi;

Naomba nianze kwa kuomba radhi kwa kutoa hotuba ya mwisho wa mwezi wa saba, leo tarehe 01 Agosti, 2012 badala ya jana tarehe 31 Julai, 2012. Hii ni kwa sababu ya msiba uliotukuta katika familia na mimi kwenda Lindi kushiriki maziko ya marehemu wetu. Tofauti na miezi iliyopita leo, pamoja na hotuba ya kawaida ya mwisho wa mwezi nimetoa fursa kwa Wahariri wa vyombo vya habari nchini kuniuliza maswali nami kujibu. Kwa upande wangu nina mambo matatu ambayo nitayazungumzia leo.

Ajali ya Kuzama kwa Meli ya MV SKAGIT

Ndugu Wananchi;

Jambo la kwanza ni ajali ya Meli ya MV SKAGIT iliyotokea tarehe 18 Julai, 2012. Meli hiyo ilikuwa na watu 290, wakiwemo mabaharia 9,abiria watu wazima 250 na watoto 31. Juhudi za uokoaji zilianza mara baada ya taarifa ya kuzama kwa meli hiyo kupatikana. Maofisa na askari wa JWTZ, Polisi na KMKM walishiriki pamoja na meli na watu binafsi katika uokoaji. Waokoaji walifanikiwa kuwapata ndugu zetu146 wakiwa hai na maiti 126 hadi tarehe 27 Julai, 2012. Kwa maana hiyo basi, watu 18 hawajulikani walipo na inahofiwa kuwa nao pia hawako hai. Huenda wamezama pamoja na meli au walizama baharini lakini miili yao haikuweza kupatikana.

Ndugu Wananchi;
Napenda kutumia nafasi hii kurudia kutoa mkono wa rambirambi na pole nyingi kwa wale wote waliopoteza ndugu, jamaa na marafiki katika ajali ile. Nampongeza sana Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mheshimiwa Dkt. Ali Mohamed Shein na viongozi wenzake wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) kwa kazi kubwa na nzuri waliofanya kuongoza juhudi za uokoaji pamoja na huduma walizotoa kwa waliokolewa, waliojeruhiwa na waliofariki. Kwa wale ambao walikuwa wenyeji wa Unguja na Pemba, SMZ ilitoa sanda na usafirishaji wa maiti mpaka makwao kwa mazishi. Kwa wale wasiokuwa na ndugu Serikali ilibeba jukumu la kuwazika kule Kama, Kusini Unguja.

Natoa pongezi za pekee kwa wale wote walioshiriki katika uokoaji kwani juhudi zao ziliwezesha ndugu zetu wengi kusalimika na maiti nyingi kupatikana.

Ndugu Wananchi;
Kutokea kwa ajali ile kumetonesha jeraha la huzuni, majonzi na mashaka makubwa yaliyolipata taifa letu miezi 11 iliyopita kufuatia ajali ya kuzama kwa meli ya MV Spice Islander. Katika mkutano maalum wa Baraza la Usalama wa Taifa niliouitisha tarehe 20 Julai, 2012 kuzungumzia ajali ya MV SKAGIT tulifanya mapitio ya utekelezaji wa maagizo yetu ya mkutano wa tarehe 11 Septemba, 2011 kufuatia ajali ya MV Spice Islander. Kwa ujumla tumeridhika kuwa utekelezaji umekuwa mzuri kwa upande wa mamlaka zinazohusika na usafirishaji majini yaani SUMATRA, Zanzibar Maritime Authority na mamlaka za Bandari za nchi zetu mbili. Ushirikiano baina ya mamlaka hizo sasa ni mzuri kwa mambo yote muhimu ambayo Baraza liliagiza wafanye hivyo. Pamoja na hayo Baraza limetaka ushirikiano huo uzidishwe na kuimarishwa.

Kwa mfano, Baraza limefurahishwa na kupongeza kitendo cha mamlaka hizo kutumia Dar es Salaam Maritime Institute kwa ushauri kuhusu ubora wa meli na huduma za usafirishaji majini. Baraza limeagiza vyombo hivyo viwe na hadidu za rejea zinazofanana kwa vigezo vya ubora ili nchi yetu iwe na viwango vinavyofanana vya ubora wa meli na huduma za usafirishaji baharini kwa pande zetu mbili za Muungano. Bahari ni moja na vyombo vinahudumia watu wale wale, kuwa na vigezo tofauti vya ubora wa meli na viwango vya huduma ni jambo lisilostahili kuwepo tena, ni la hatari. Baraza pia limeagiza pawepo na ukomo wa umri wa meli zilizokwishatumika zinazoruhusiwa kutumika hapa nchini.

Aidha, Baraza limerudia kuagiza pawepo na usimamizi makini zaidi kuhusu upakiaji wa mizigo na abiria. Mamlaka husika, yaani SUMATRA, ZMA na maofisa wa bandari wahakikishe kuwa uwezo wa meli uliohakikiwa na kutambuliwa unaheshimiwa ipasavyo. Pia, meli zikaguliwe mara kwa mara na vigezo vifanane.

Ndugu Wananchi;
Pamoja na hayo, Baraza la Usalama wa Taifa limeona kuwa wakati umefika kwa Serikali yetu kuwa na Coast Guards, yaani kikosi maalum cha uokoaji na usalama majini. Aidha, Baraza limetaka hatua za makusudi zichukuliwe kuimarisha KMKM na Police Marines. Mwisho, Baraza lilipongeza uamuzi wa SMZ wa kuunda Tume ya kuchunguza ajali ile kama ilivyofanya wakati wa ajali ya MV Spice Islander.

Utafutaji na Uchimbaji Gesi Nchini

Ndugu Wananchi,

Jambo la pili ninalopenda kulizungumzia leo ni kuhusu maendeleo ya sekta ya gesi asili nchini. Juhudi za kutafuta mafuta nchini zilianza mwaka 1952 na mwaka 1954 wakati kampuni ya BP ilichimba kisima cha kwanza kule Mafia. Bahati mbaya kisima hicho hakikuzaa matunda yaliyotarajiwa na juhudi za utafutaji mafuta zikafifia kabisa mwanzoni mwa miaka ya 1960. Miaka kumi baadae, juhudi hizo zilianza upya na kuendelea kwa kiwango na kasi za namna mbalimbali hadi sasa. Katika miaka ya hivi karibuni juhudi zimekuwa kubwa na kuhusisha makampuni kadhaa ya kimataifa yakiwemo makubwa na madogo.

Ndugu Wananchi;
Tangu mwaka 1954, mpaka sasa visima 61 vimechimbwa, kati ya hivyo, gesi asili imegunduliwa katika visima 22, visima 14 vya nchi kavu na maeneo ya maji mafupi na visima 8vya bahari ya kina kirefu. Hatujabahatika kupata mafuta lakini tumefanikiwa kupata gesi asili katika maeneo kadhaa baharini na nchi kavu katika mikoa ya Mtwara, Lindi na Pwani.

Kwa mujibu wa taarifa zilizopo kutokana na visima vilivyochimbwa mpaka sasa, akiba ya gesi asili iliyopo nchini inakadiriwa kuwa kati ya futi za ujazo trilioni 25.4 – 28.9. Yapo matumaini makubwa ya gesi nyingi zaidi kugundulika katika miaka michache ijayo. Hii ni kutokana na ukweli kwamba shughuli za utafutaji mafuta na hasa gesi baharini zilizoanza mwaka 2004 kukiwa na kampuni moja sasa zipo 18. Baada ya ugunduzi wa kwanza wa gesi mwaka 2010, shughuli za utafutaji sasa zimepamba moto na zimekuwa na mafanikio. Naamini gesi nyingi zaidi itaendelea kupatikana.

Fursa za Maendeleo

Ndugu Wananchi;

Kwa kiasi cha gesi asili kilichokwishagunduliwa na kwa matumaini yaliyopo ya gesi zaidi kupatikana kunaifanya Tanzania kuwa moja ya nchi za kutumainiwa duniani kwa upatikanaji wa gesi asili miaka michache ijayo. Hali hiyo inaipa nchi yetu fursa kubwa ya kuweza kujiletea maendeleo makubwa ya kiuchumi na kijamii muda si mrefu kutoka sasa.

Gesi asili ni rasilimali inayoweza kutumika kuzalisha mbolea na hivyo kusaidia katika kuendeleza kilimo nchini kwa kurahisisha upatikanaji wake na kuwa ya bei nafuu. Gesi asili inaweza kutumika kuzalisha umeme na hivyo kuiwezesha nchi kupata umeme wa kutosha na kuwepo ziada ya kuuza nje. Hivi sasa, katika gridi ya taifa megawati 350za umeme zinatokana na gesi asili na hata lengo letu la kuzalisha megawati 3,500 ifikapo maka 2015 tunategemea zaidi gesi asili kuwezesha hilo kutimia. Ujenzi wa bomba la gesi kutoka Mtwara kuja Dar es Salaam una shabaha hiyo.

Ndugu Wananchi;
Vile vile, gesi asili inaweza kutumika kutoa nishati viwandani badala ya kutumia mafuta na hivyo kupunguza gharama za uzalishaji. Watu majumbani wanaweza kutumia gesi asili kupikia hivyo kupunguza matumizi ya umeme, mafuta, mkaa na kuni. Inapunguza gharama za maisha na kusaidia kuhifadhi mazingira kwa kupunguza ukataji wa miti. Ni kutokana na kutambua ukweli huo ndiyo maana TPDC inatekeleza mradi wa kutengeneza gridi ya mabomba ya kusambaza gesi majumbani katika jiji la Dar es Salaam.

Jambo lingine muhimu kuhusu rasilimali hii ni kwamba tukiuza nje gesi nchi yetu itapata mapato mengi tena ya fedha za kigeni. Kwa vile gesi ni nyingi mapato ya Serikali yataongezeka sana, hivyo kuijengea uwezo wa kutimiza majukumu yake vizuri zaidi. Kama matumizi yatakuwa mazuri, gesi asili itakuwa kichocheo kikubwa cha kukuza uchumi wa nchi. Maendeleo ya haraka yatapatikana na hivyo kusaidia kuwaondoa wananchi wengi kutoka katika lindi la umaskini tulionao sasa.

Changamoto Muhimu

Ndugu Wananchi;

Pamoja na ukweli kwamba kuwa na gesi asili nyingi kunaipa nchi yetu fursa kubwa ya kujiletea maendeleo, zipo pia changamoto zake. Hatuna budi kuzitambua na kuzitafutia ufumbuzi ili gesi iweze kunufaisha ipasavyo nchi yetu na watu wake. Changamoto zipo nyingi lakini kubwa zipo za namna tatu.

Changamoto ya kwanza ni ile ya kujenga uwezo wetu wenyewe wa kudhibiti shughuli zinazofanywa na makampuni ya mafuta ili tuhakikishe kuwa tunapata malipo yanayostahili. Inatulazimu tuwe na wataalamu wetu wazalendo wa fani za taaluma zihusuzo gesi kama vile uhandisi, kemia, jiofizikia, uhasibu, ukaguzi na sheria. Tusipojenga uwezo wetu wenyewe kwenye maeneo hayo kuna hatari ya kudhulumiwa na kupata hasara. Pengine ipo haja ya kuwa na chombo maalum kwa ajili hiyo kama tulivyofanya kwa mafanikio kwa upande wa dhahabu.

Changamoto ya pili ni ile ya kupata Watanzania wengi wenye ujuzi na taaluma zinazohitajika na soko la ajira la sekta ya gesi. Tusipofanya hivyo makampuni yataajiri watu hao kutoka nje na hivyo kufanya Watanzania kutokunufaika na fursa za ajira zilizopo.

Ndugu Wananchi,
Kwa changamoto hizi mbili, jawabu lipo kwenye elimu na mafunzo tunayotoa kwa vijana wetu katika shule, vyuo vya ufundi na vyuo vya elimu ya juu. Kwanza kabisa lazima tuboreshe elimu ya sayansi na hisabati katika shule zetu za msingi na sekondari. Katika vyuo vya ufundi tutoe mafundi mchundo wa taaluma zinazohitajika na tasnia ya gesi na mafuta. Hivyo hivyo kwa upande wa vyuo vikuu nako wafundishe wataalamu wa fani zinazohitajika kama vile utafutaji wa gesi na mafuta, uendelezaji wa mafuta na gesi, uchumi na biashara ya mafuta na gesi, uhasibu na ukaguzi wa mafuta na gesi pamoja na sheria za mafuta na gesi na mikataba ya utafutaji na uendelezaji wa mafuta na gesi.

Ndugu Wananchi;
Napenda kuwahakikishia kuwa tayari tumejipanga kutafuta ufumbuzi wa changamoto hizo. Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kinajiandaa kuanza kutoa mafunzo ya Chemical and Environmental Lab for Oil and Gas na fani ya Exploration and Production Software Technologykatika mwaka huu wa masomo. Chuo cha Madini Dodoma kitaanza kutoa mafunzo ya diploma ya Petroleum Geoscience kuanzia Septemba mwaka huu. Chuo Kikuu cha Dodoma, Chuo cha Sayansi na Teknolojia cha Nelson Mandela Arusha, na Chuo cha Teknolojia cha Mbeya na kile cha Dar es Salaam pia wameanza kufundisha mitaala hiyo. Aidha, VETA Makao Makuu na VETA Mtwara nao wanafundisha masomo yahusuyo gesi. Wizara ya Nishati na Madini itawadhamini wanafunzi 50 kutoka Mkoa wa Mtwara kwenda kupata mafunzo hayo ya gesi asili katika chuo cha VETA Mtwara.

Ndugu Wananchi;
Wizara ya Nishati na Madini pia inatekeleza mpango mkakati wa kuwapata wataalamu wa sekta hiyo kati ya 40-50 kati ya sasa na mwaka 2016. Taaluma zinazotiliwa mkazo ni Petroleum Geoscience, Petroleum Geophysics, Petroleum Geochemistry, Petroleum Engineering, Petroleum Modeling, Oil and Gas economics, Oil and Gas Accounting and Auditing na Oil and gas Legal Regimes and Contract Negotiations. Kwa upande wake, Serikali itatoa upendeleo maalum kwa kulipia gharama zote za mafunzo ili tuweze kuwapata wataalamu hawa mapema iwezekanavyo. Nawaomba vijana wetu wachangamkie fursa hizi za masomo na watakapohitimu mafunzo wawe tayari kuitumikia nchi yetu kwa bidii.

Kujenga Uwezo Wetu wa Kutumia Mapato ya Gesi

Ndugu Wananchi,
Changamoto nyingine kubwa sana ni ile ya kuhakikisha kuwa mapato yatokanayo na gesi yanatumika vizuri na kwa manufaa ya taifa na watu wake. Lazima tuanze sasa kufikiria na kujipanga kwa ajili hiyo. Si vyema tukangojea mpaka hapo mapato yatakapoanza kupatikana ndiyo tufikirie na kutengeneza mfumo mzuri wa kusimamia na kutumia mapato yatokanayo na gesi. Tutakuwa tumechelewa, watu laghai na waovu watakuwa wameanza kunufaika hivyo watakuwa wagumu kutengeneza mfumo utakaowanyima fursa ya kuliibia taifa.

Jambo hili ni muhimu sana kufanya kwani ipo mifano hai ya nchi zenye rasilimali nyingi za mafuta na gesi lakini nchi na wananchi wake hawanufaiki sawia. Mauzo yanafanyika na fedha nyingi kupatikana lakini manufaa kwa nchi na watu wake ni madogo au hayapo kabisa. Wanaonufaika ni viongozi na baadhi ya maofisa wa umma wanaohusika na usimamizi wa shughuli zihusuzo rasilimali hizo. Na, hata sisi tunaweza kujikuta katika hali hiyo kama tusipojipanga vizuri sasa ambayo badala ya rasilimali kuwa baraka zinageuka kuwa balaa au hata laana.

Ndugu Wananchi;
Zipo nchi duniani ambazo zina usimamizi mzuri wa mapato ya rasilimali za mafuta na gesi na kuleta baraka na neema kwa taifa na watu wake. Nchi hizo zimeweza kuhifadhi na kutumia vizuri mapato yake kukuza uchumi wa nchi kwa jumla na kuboresha upatikanaji wa huduma za kiuchumi na kijamii kwa watu. Matokeo yake ni watu wa nchi hizo kuishi maisha yaliyo bora kuliko walivyokuwa kabla ya kupatikana kwa rasilimali hizo. Lakini, hii imewezekana kutokana na usimamizi mzuri na matumizi mazuri ya mapato yatokanayo na mafuta na gesi.

Tumeamua kujifunza kutoka nchi za wenzetu waliofanikiwa ili na sisi tunufaike. Na sisi tunajiandaa kutengemeza Sera ya Gesi Asili na kurekebisha Sheria ya Utafutaji na Uzalishaji wa Mafuta na Sheria ya Menejimenti ya Mapato ya Serikali yatokanayo na gesi zitakazotoa majibu hayo na kuliwezesha taifa kuwa na mfumo mzuri wa usimamizi wa utafutaji na uchimbaji wa gesi asili pamoja na usimamizi na matumizi mazuri ya mapato yatokanayo na gesi hiyo. Wapo wenzetu kwa mfano, wanacho kitu kinachoitwa Sovereign Funds ambapo mapato yote huhifadhiwa na baadae hutolewa kwa utaratibu maalum.

Tunataka tujifunze kutoka kwao ili na sisi tutengeneze chombo chetu cha namna hiyo ili tunufaike.

Ndugu Wananchi;
Mambo hayo tumeshaanza kuyafanyia kazi. Katika mazungumzo yangu na baadhi ya wakuu wa nchi rafiki na mashirika ya maendeleo ya kimataifa, nimewasilisha maombi ya kusaidiwa na kushirikiana kwa mambo mawili. Kwanza kwa kuwawezesha Watanzania kupata mafunzo ya haraka kwa wataalamu watakaosaidia kusimamia shughuli za utafutaji, uendelezaji na biashara ya gesi asili nchini. Pili, watusaidie kupata watu wenye ujuzi na uzoefu ili watushauri kuhusu namna ya kutengeneza mifumo bora ya kusimamia na kutumia mapato ya gesi kwa mujibu wa mifano ya wenzetu waliofanikiwa.

Nafurahi kwamba maombi yetu yamepokelewa vizuri na nchi zote na mashirika yote ya kimataifa tuliozungumza nao. Baada ya muda si mrefu kazi itaanza.

Mgomo wa Walimu

Ndugu Wananchi;
Jambo la tatu na la mwisho ni mgomo wa walimu. Pengine ni mapema kusema kwa vile kesho Mahakama itaamua kuhusu shauri hilo. Lakini napenda kuwahakikishia walimu kuwa tunawajali, tunawathamini na kutambua mchango wao muhimu kwa taifa letu. Wakati wote tumekuwa tunashughulikia madai ya haki zao na malimbikizo mbalimbali. Madai ya safari hii ni makubwa mno, yametuzidi kimo. Athari za kuyatimiza yalivyo yataifanya bajeti ya Serikali kutumia asilimia 75kwa ajili ya mishahara ya watumishi wa Serikali na kubakiza asilimia 25kwa kuendeshea Serikali na kutimiza majukumu ya maendeleo kwa wananchi. Haitakuwa sawa. Ndiyo maana tumeshindwa kuelewana walipokataa rai hiyo na wao kusisitiza kugoma.

Wakati tunaendelea kusubiri uamuzi wa Mahakama, nina maombi mawili kwa walimu: Moja, wasiwalazimishe walimu wasiotaka kugoma wafanye hivyo, wawaache waendelee na kazi. Pili, wasitumie watoto isivyostahili kujenga hoja zao. Nawasihi warudi kwenye meza ya mazungumzo.

Ndugu Wananchi;
Kabla ya kumaliza hotuba yangu naomba nitumie fursa hii kuwatakia Waislamu wote nchini kheri na baraka tele kwa swaumu ya mwezi mtukufu wa Ramadhan. Wakati wote, mjiombee wenyewe kwa Mwenyezi Mungu awajaalie toba na malipo mema katika mfungo huu. Mkumbuke pia kuiombea nchi yetu amani, upendo na mafanikio mema.

Baada ya maneno hayo, naomba sasa niishie hapo. Nawashukuru sana kwa kunisikiliza.

Wakimbizi Wa Burundi Wavuliwa Hadhi Ya Ukimbizi

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Serikali, kuanzia tarehe 01 Agosti, 2012, imewavua hadhi ya ukimbizi wakimbizi 38,050 wa kutoka Burundi wanaohifadhiwa katika kambi ya wakimbizi ya Mtabila iliyoko wilayani Kasulu mkoani Kigoma.Uamuzi huu wa kuwavua hadhi ya ukimbizi umefanywa na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Dk. Emmanuel Nchimbi kwa Mamlaka aliyopewa chini ya Kifungu cha 4 cha Sheria ya Wakimbizi.

Kufuatana na Sheria hiyo mkimbizi anapoteza hadhi ya ukimbizi kama mazingira yaliyomfanya kuwa mkimbizi yatakuwa hayapo tena, na atavuliwa hadhi hiyo kama ataendelea kukaidi maagizo halali ya kumtaka kurejea kwao kwa hiari.

Hatua ya kuwavua hadhi ya ukimbizi wakimbizi hawa imefikiwa baada ya Serikali za Tanzania na Burundi na Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Wakimbizi (UNHCR) kujiridhisha kuwa hapakuwa tena na sababu ya kuendelea kuwahifadhi wakimbizi hao baada ya hali ya amani kurejea nchini mwao na hivyo kuwataka kurejea kwao.

Zoezi la kuwasaili wakimbizi waliopo katika kambi ya wakimbizi ya Mtabila lilifanyika kuanzia mwezi Septemba hadi Desemba mwaka 2011 kwa lengo la kubaini kama walikuwepo wakimbizi wenye sababu za msingi za kuendelea kuwepo nchini, ambapo ilibainika kuwa wakimbizi 38,050 hawakuwa na sababu za kuendelea kuwa wakimbizi.

Kufuatia matokeo ya zoezi hilo, Kikao cha Pande Tatu, kilichojumuisha wawakilishi wa Serikali za Tanzania na Burundi na Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Wakimbizi (UNHCR), kilifanyika jijini Bujumbura nchini Burundi tarehe 22 Februari, 2012 na kukubaliana kwa pamoja kuifunga kambi ya Mtabila ifikapo tarehe 31 Desemba, 2012.

Baada ya kuwavua hadhi ya ukimbizi, raia hawa wa Burundi sasa wataendelea kusaidiwa kurejea kwao kwa hiari hadi tarehe 31 Desemba mwaka huu, ambapo Kambi hiyo ya Mtabila itafungwa rasmi, na wale ambao watakuwa hawajaondoka baada ya tarehe hiyo watachukuliwa kuwa ni wahamiaji haramu, na kushughulikiwa kufuatana na Sheria ya Uhamiaji.

Historia ya hifadhi ya wakimbizi hapa nchini ilianza tangu mwaka 1961 ambapo Tanzania ilikuwa na idadi kubwa ya wakimbizi kutoka nchi mbalimbali za Afrika, idadi ambayo katika miaka ya tisini ilifikia takribani milioni moja, 641,386 kati yao wakiwa ni wakimbizi kutoka Burundi.

Zoezi la kuwarejesha kwao wakimbizi wa Burundi lilianza rasmi mwaka 2002 baada ya nchi yao kurejea katika hali ya amani na hadi sasa kambi nane zilizokuwa zikihifadhi wakimbizi toka Burundi zimefungwa. Kambi hizo ni Karago, Mtendeli, Kanembwa na Nduta zilizokuwa wilayani Kibondo, na Muyovosi iliyokuwa wilayani Kasulu, mkoani Kigoma.

Kambi nyingine zilizofungwa ni Kitali iliyokuwa wilayani Biharamulo, Lukole A na B zilizokuwa wilayani Ngara, mkoani Kigoma.Kambi ya wakimbizi ya Mtabila ndiyo itakuwa ya mwisho kufungwa katika mlolongo wa kambi zilizokuwa zikihifadhi wakimbizi kutoka Burundi hapa nchini.

Imetolewa na Isaac J. Nantanga:
MSEMAJI WA WIZARA YA MAMBO YA NDANI YA NCHI

Taarifa Kwa Umma

P.O. Box 78172, Phone: 2137547/8, Fax: 2137548, E-Mail: info@misatan.org, Dar es Salaam, Tanzania.

TAARIFA KWA UMMA
Taasisi ya vyombo vya habari Kusini mwa Afrika tawi la Tanzania MISA-Tanzania) inasikitika kuarifu umma wa watanzania kwamba inapinga vikali kitendo cha serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Ofisi ya Msajili wa Magazeti Tanzania Bara kulifungia kutochapishwa kwa muda usiojulikana gazeti la MwanaHalisi kuanzia tarehe 30 Julai 2012.

Katika taarifa iliyotolewa na serikali kupitia tangazo lake lililochapishwa kwenye magazeti mbalimbali hapa nchini na kunukuu kutolewa kwa amri hiyo kupitia gazeti la serikali (Government Notice) toleo namba 258 la tarehe 27 Julai 2012, serikali imeeleza kama ifuatavyo:

“Serikali imeamua kulifungia kutochapishwa kwa muda usiojulikana gazeti la MwanaHalisi kwa mujibu wa sheria ya Magazeti ya mwaka 1976, kifungu namba 25 (i), adhabu hiyo itaanza tarehe 30 Julai 2012”

Aidha, tamko hilo la serikali limeeleza pia kuwa sababu za msingi za kulifungia gazeti hilo ni kufuatia machapisho mbalimbali ya gazeti hilo kwenye toleo Na. 302, Na. 303 pamoja na toleo Na. 304 yote yakiwa ya mwezi Julai 2012 pamoja na machapisho mengine yaliyotangulia. Serikali imeeleza kuwa machapisho hayo yamekuwa “yakichapisha habari na makala zenye kueneza na kujenga hofu kwa jamii”

Hata hivyo, serikali haikubainisha ni habari zipi katika machapisho hayo ambazo zinaeneza na kujenga hofu kwa jamii. Kitendo hicho cha kutobainisha habari husika kinatufanya sisi kama wanahabari na watetezi wa haki ya kupata taarifa pamoja na uhuru wa vyombo vya habari nchini na katika kanda ya kusini mwa Afrika kutoridhia maamuzi ya serikali kwani yamehusisha masuala ambayo hayakuwekwa bayana.

Ni kwa mashaka makubwa ambayo yanatokana na tamko husika la serikali kwa kutumia maneno yafuatayo:

“Kuanzia sasa serikali haitasita kuchukua hatua dhidi ya vyombo vya habari ambavyo kwa makusudi vitatoa taarifa za uchochezi ambazo zitahatarisha hali ya amani na utulivu uliopo nchini mwetu”

MISA–Tanzania inasikitishwa na kauli hiyo kwani kauli hiyo ni kudhihirisha matumizi mabaya ya sheria zilizopo katika kukandamiza uhuru wa kupata taarifa na uhuru wa vyombo vya habari kinyume na matakwa ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 ibara ya 18 (b) na (d) kama ilivyofanyiwa marekebisho mwaka 2005.

Haki ya kutafuta, kupata na kutoa taarifa ni haki ya msingi ya kila binadamu na imetambuliwa hivyo na Katiba ya Tanzania. Haki hii imetambuliwa pia na mikataba mbalimbali ya Kimataifa ambayo Tanzania imeiridhia bila masharti yoyote.

Kama kweli kuna taarifa za uchochezi zilizochapishwa na gazeti la MwanaHalisi na kuhatarisha amani na utulivu wa nchi, ni vyema serikali ingebainisha taarifa hizo kwenye chapisho husika na siyo kuorodhesha machapisho mbalimbali kama sababu yake ya kulifungia gazeti. Hata hivyo, mamlaka ya serikali kufungia gazeti kupitia msajili wa magazeti ni ukiukwaji wa misingi ya haki za binadamu na matumizi makubwa ya madaraka.

Ni kwa sababu hizo kwamba Ripoti ya Haki za Binadamu iliyowahi kuandaliwa na kutolewa na Tume maalumu iliyoundwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kujulikana kama Tume ya Jaji Nyalali mwaka 1992 ilibainisha sheria ya Magazeti ya mwaka 1976 kuwa ni miongoni mwa sheria arobaini ambazo zinakandamiza haki za binadamu nchini. Sheria hiyo haina budi kufutwa kwenye vitabu vya sheria za nchi hii.

Kitendo cha kulifungia gazeti la MwanaHalisi kwa muda usiojulikana kinaweza kusababisha hofu kubwa kwa watetezi wa haki za binadamu na wanahabari kwa ujumla. Kitendo hicho kinafuatia kile cha kuwakamata na kuwaweka rumande (Oysterbay Polisi) wanaharakati zaidi ya kumi kwa tuhuma mbalimbali ikiwamo kuandamana kufuatia mgomo wa Madaktari mnamo tarehe 9 mwezi Februari 2012.

MISA –Tanzania inalaani vikali matumizi mabaya ya Dola katika kunyamazisha wanahabari wanapojaribu na kuthubutu kufuatilia matukio mbalimbali na kuarifu umma kuhusu yale waliyoyafanyia kazi kwa kina. Ni rai yetu kwa serikali kuwa ni vyema wabainishe taarifa mahsusi zilizopelekea maamuzi ya kufungia gazeti la MwanaHalisi ili kutuondolea hofu sisi tunaotetea haki na uhuru wa vyombo vya habari. Kuendelea kuficha taarifa husika ni kuendelea kuikanyaga Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, 1977 (ibara ya 18) kupitia kivuli cha Sheria ya Magazeti ya mwaka 1976 ambayo kimsingi imepitwa na wakati na haiwezi kutumika kinyume na Katiba ya nchi.

Ni rai yetu pia kwa serikali ya Tanzania kwamba izingatie Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika yale yenye kuhamasisha utoaji haki kuliko kujikita kwenye kifungu cha 30 cha Katiba hiyo ambacho kimsingi kinaweka mipaka maalumu ya ukiukwaji wa haki za binadamu. Mipaka hiyo haionekani kuzingatiwa na serikali katika kulifungia gazeti la MwanaHalisi.

Kwa taarifa hii kwa umma, tunaiomba pia serikali ya jamhuri ya Muungano wa Tanzania kulifungulia gazeti la MwanaHalisi mapema iwezekanavyo na bila masharti ili kuwawezesha watanzania kuendelea kunufaika na taarifa zinazochapishwa na gazeti hilo ilmradi maadili ya uandishi wa habari yazingatiwe. Hii ni haki ya msingi kwa kila mtu na ni vyema aione ikitekelezeka.

Taarifa hii imetolewa na kusaini hapa Dar es salaam tarehe 31 Julai 2012.

………………………….
Mohammed Tibanyendera
Mwenyekiti, MISA-TAN

Bungeni

 Waziri wa Uchukuzi Dkt. Harrison Mwakyembe akielekea ndani ya ukumbo wa Bunge mjini Dodoma Aug,1,2012 kwaajili ya kusoma Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Uchukuzi kwa mwaka wa Fedha,2012-2012
 Waziri wa Nchi , Ofisi ya Rais- Asiye na Wizara Maalumu Prof, Mark Mwandosya akitoa shukurani Aug,1,2012 kwa Serikali na Wananchi waliomuombea wakati akiwa mgojwa hadi kupata nafuu na kuweza kuhudhuria tena katika vikao vya Bunge ,mjini Dodoma.
 Naibu Waziri wa Katiba na Sheria Angellah Kairuki akijibu hoja mbalimbali  Bungeni leo kuhusu wizara yake,
Mbunge wa Kigoma Kaskazini Kabwe Zitto (kulia) akitoa maelezo binafsi kwa waandishi  wa habari Aug. 1,2012 kuhusu tuhuma za rushwa dhidi yake hususan kuelekea katika kupitisha bajeti ya Wizara ya Nishati. Pichani mwengine ni  Prof. Koyela Kahigi (CHADEMA). Picha na Mwanakombo Jumaa- MAELEZO,

Tuhuma Za Rushwa: Utetezi Wa Zitto Kabwe

MAELEZO BINAFSI YA MHE. ZITTO ZUBERI KABWE DHIDI YA TUHUMA ZA RUSHWA HUSUSAN KUELEKEA KATIKA KUPITISHA BAJETI YA WIZARA YA NISHATI NA MADINI
Ndugu Waandishi,

Nalazimika kukutana nanyi kutoa maelezo juu ya tuhuma zenye shinikizo la kisiasa zinazoelekezwa kwangu binafsi kwamba hata mimi nimeshiriki katika vitendo vya rushwa, kwa nafasi yangu kama Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Mashirika ya Umma. Taarifa hizo, kama kawaida ya uzushi mwingine wowote zimesambazwa kimkakati na kwa kasi kubwa kiasi cha kuukanganya umma.

Nafahamu nabeba dhamana kubwa ya uongozi, taswira yangu ya uongozi daima imeakisi njozi na matumaini ya wananchi wa Kigoma Kaskazini, wananchi wanyonge na vijana kote nchini bila kujali itikadi zao za kisiasa, jinsia zao, makabila yao na rika zao. Hivyo, nawajibika kupitia kwenu kuwatoa hofu juu ya hisia potofu zinazopandikizwa kwao na wale wasiopenda kuona baadhi yetu tukiwaunganisha na kuwasemea watanzania wasio na sauti, dhidi ya vitendo vya hujuma na vyenye dhamira ovu kwa taifa.

Mkakati huo wa kuniunganisha na baadhi ya Waheshimiwa Wabunge wanaotuhumiwa kwa kupokea Rushwa unatekelezwa kwa njia zifuatazo:

Kumekuwa na kauli za watendaji wa serikali ambao wamekuwa wakizieneza na hususan kutoa taswira kwamba baadhi ya kauli zangu zinatokana na ushawishi wa rushwa;
   
Kuna taarifa ambazo zimeandikwa tena katika kurasa za mbele za baadhi ya vyombo vya habari zikidai ’’Zitto kitanzini’’ ama ’’Zitto sawa na popo nundu’’ zikiashiria kwamba na mimi ni mla rushwa; na
   
Waandishi wa habari na jamii kwa ujumla wamefikia kuaminishwa habari hizi kiasi cha wengine kuuliza kwa nini Mhe. Zitto Kabwe hakutajwa katika orodha iliyotolewa na Mnadhimu Mkuu wa Kambi ya Upinzani.

Ndugu Waandishi,
Naomba kutoa ufafanuzi wa hicho kinachoelezwa kwamba nina ushiriki katika masuala ya rushwa hususan kwenye masuala yanayohusu sekta ya Nishati na Madini:-

Mara baada ya bodi ya Wakurugenzi ya Shirika la Usambazaji wa Umeme Tanzania (TANESCO) chini ya Uenyekiti wake Meja Jenerali Mstaafu Robert Mboma kutangaza kwamba imemsimamisha kazi Mkurugenzi Mkuu wa Shirika hilo, Nd. William Mhando ili kupisha uchunguzi wa baadhi ya vitendo/mwenendo wake, Kamati ya Hesabu za Mashirika ya Umma (POAC) ambayo mimi ni Mwenyekiti wake ilimuandikia Mhe. Spika kumuomba aridhie ili Kamati iweze kuwaita Bodi ya TANESCO, Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Mahesabu ya Serikali (CAG) na pia Mamlaka ya Udhibiti wa Manunuzi ya Umma (PPRA) kujiridhisha na tuhuma zote zinazotajwa zinafanyiwa uchunguzi wa kina na hatua kuchukuliwa;
   
Kamati ya POAC ninayoiongoza ilimuomba Mhe. Spika kuwaita wahusika tajwa kwa kuwa zilikuwapo tetesi kuwa kusimamishwa kazi kwa Mkurugenzi huyo siku chache kabla ya Bajeti ya Wizara ya Nishati na Madini kulikuwa na lengo la kufunika ’madudu’ makubwa zaidi kwa kulichagiza Bunge na tukio hilo dogo, mkakati ambao naona umefanikiwa sana. Isitoshe, Kamati kutaka kujiridhisha na hatua za Bodi ni sehemu ya msingi ya utekelezaji wa majukumu ya Kamati yaliyowekwa kwa mujibu wa Kanuni za Kudumu za Bunge na pia Shirika la TANESCO ni moja kati ya mashirika ambayo yanawajibika kwetu kwa hesabu zake na pia ufanisi wake kwa ujumla. Tumefanya hivyo pia katika mashirika mengine, hili la TANESCO sio tukio la kipekee;
   
Kitendo hiki cha halali na kwa mujibu wa Kanuni kilichofanywa na Kamati yangu kimetafsiriwa kwa makusudi na baadhi ya watu kwamba ni ishara ya kuwa sisi au zaidi kwamba mimi nina maslahi binafsi na TANESCO na hususan Mkurugenzi wake Injinia Mhando, ndio maana tumetaka maelezo ya Bodi. Ukweli kwamba Kamati ya POAC tumewaita pia Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Mahesabu (CAG) na Mamlaka ya Udhibiti wa Manunuzi ya Umma (PPRA) kwa jambo hilo hilo umefichwa kwa makusudi!
   
Baada ya tukio hilo, nikiwa hapa Dodoma, mwandishi wa habari wa gazeti moja alinifuata akiniambia kuwa wamekutana na Mhe. Waziri Mhongo na Katibu Mkuu wake, Nd. Eliachim Maswi hapa hapa Bungeni na wamewaambia kuwa mimi nimepewa rushwa. Hakutaja nimepewa rushwa na nani, kiasi gani na wala kwa lengo gani!
   
Nimejaribu kumtafuta kwa simu Mhe. Waziri Mhongo na Katibu Mkuu wake ili wanipe ufafanuzi juu ya mimi na Kamati ya POAC kuhusishwa na tuhuma hizi bila mafanikio, hali ambayo inaniondolea mashaka juu ya ushiriki wao katika kueneza au kuthibitisha uvumi huo. Najaribu sana kujizuia kutokuwa na mashaka na ushiriki wao huo ikizingatiwa uzito na taswira ya nafasi zao katika jamii, lakini wameshindwa kunidhihirishia tofauti Sasa naomba kutoa ufafanuzi rasmi kuhusu mlolongo wa matukio hayo tajwa ambayo yanatumiwa na baadhi ya wanasiasa kuonesha kwamba eti nimehusika na vitendo vya rushwa.

Binafsi sijawahi kuwa na mawasiliano ya aina yeyote na uongozi wa TANESCO kushawishiwa juu ya hatua ambazo POAC ndio imezichukua za kutaka kujiridhisha juu ya utaratibu uliotumika. Ieleweke wazi kabisa kuwa, hakuna wakati wowote, popote ambapo mimi binafsi au Kamati yetu imekataa Mkurugenzi Mkuu wa TANESCO kuchunguzwa kwa tuhuma zozote. Ambacho tumesisitiza wakati wote ni ufuatwaji wa taratibu, kanuni na sheria, hili nitalisimamia iwe masika au kiangazi;
   
Ni kwa sababu hiyo, na kwa kujiamini kabisa nimeunga mkono suala la tuhuma za rushwa zinazotajwa zichunguzwe na Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge kwa kina;
   
Nimekwenda mbali zaidi kukiomba chama changu CHADEMA kifanye pia uchunguzi na tathmini yake kwa kina kujiridhisha na tuhuma hizo;
   
Natumia fursa hii pia kuomba vyombo vya Dola vichunguze tuhuma hizo kwa nafasi yake ili kuweza kupata ukweli;
   
Ninaahidi kushiriki kikamilifu iwapo nitatakiwa katika uchunguzi wowote utakaofanywa na niko tayari kuwajibika iwapo nitakutwa na hatia yeyote.

Napenda niwatoe hofu wananchi wa jimbo la Kigoma Kaskazini walionituma kuja kuwawakilisha hapa Bungeni na Watanzania wote kwa ujumla kwamba:-

Mimi Zitto Zuberi Kabwe sina bei, sijawahi kuwa nayo na sitarajii kuwa nayo huko mbeleni. Daima nimesimamia kidete maadili ya uongozi bora katika maisha yangu yote ya siasa, na nawaahidi sitarudi nyuma katika mapambano dhidi ya rushwa katika nchi hii pamoja na mikakati ya aina hii ya kunidhoofisha na kunivunja moyo;
   
Nafarijika na salam mbali mbali zinazotolewa kunifariji na kusisitiza kuwa nisilegeze kamba katika mapambano haya, nimepokea ujumbe mwingi kwa simu, sms, tweeter na hata facebook na niko pamoja nanyi Watanzania wenzangu kamwe sitarudi nyuma hadi kieleweke. Naamini katika nchi yetu tunazo rasilimali za kutosha mahitaji/haja ya kila mmoja wetu lakini si ‘tamaa/ulafi’ wa baadhi ya watanzania wenzetu;
   
Napenda kuweka rekodi sawa kwa Watanzania kwamba nimekuwa Mbunge hiki ni kipindi cha pili, Mimi ni Mwenyekiti wa Kamati ya Hesabu za Mashirika ya Umma (POAC) huu ni takriban mwaka wa saba sasa, Kamati yangu inasimamia mashirika 259 ya Umma na si TANESCO peke yake. Mchango wa Kamati hii katika Bunge na kwa ustawi wa Mashirika ya Umma ni bayana na haujawahi kutiliwa shaka. Kamati yetu imeokoa upotevu mkubwa wa mali za umma na kuokoa fedha za umma kutokana na umakini wake. Tumefanya hivyo CHC hivi karibuni, Kiwira na kwenye mashirika mengine mengi. Kote huko uadilifu na uzalendo wa Kamati hii haujawahi kuhojiwa. Inatuwia vigumu kuona kuwa tunahojiwa katika suala hili la TANESCO. Hapa pana kitendawili.
   
Zipo hoja pandikizi za kutaka Kamati ya POAC ivunjwe na haswa zikinilenga mimi binafsi. Nafahamu kiu ya wasioitakia mema nchi yetu kuiona POAC ikivunjwa au sura zikibadilishwa kwa kuwa Kamati hii imekuwa mwiba kwa mikakati yao ya kifisadi. Kwa maoni yangu, Kamati ya POAC isihusishwe na tuhuma hizi kwa vyovyote vile. Niko tayari nihukumiwe mimi kama mimi na sio kuhusisha wajumbe wengine ambao hawatajwi mahala popote katika tuhuma hizi mbaya sana katika historia ya Bunge letu. Nitakuwa tayari kunusuru Kamati ya POAC na maslahi ya taifa letu kwa kujiuzulu Uenyekiti iwapo itathibitika pasipo shaka kuwa nimehongwa. Kamati ya POAC ni muhimu zaidi kuliko mimi.
   
Nafahamu pia kuwa kuna wanasiasa hasa wa Upinzani ambao wanautaka sana Uenyekiti wa POAC na wanafanya kila njia kutaka kuidhoofisha. Lakini hawajui kuwa anaepanga wajumbe wa Kamati ni Spika wa Bunge.
   
Msishangae pia kuja baadae kubaini kwamba baadhi ya wanasiasa wenye midomo mikubwa ya kutuhumu wenzao wao ndio vinara wa kupokea rushwa.
   
Ni lazima tufike mahali kama viongozi kwamba utaratibu unapokiukwa na yeyote yule, au uongo unapotolewa hadharani tuseme bila kuogopa. Hili ndio jukumu letu kama wabunge na viongozi. Kusimamia ufuatiliaji wa utaratibu ni jukumu letu kama Kamati ya POAC na ndio sababu ya msingi ya kuanzishwa kwa mamlaka kama CAG na PPRA. Haiwezekani, tuwe na set ya kanuni kwa kundi fulani na nyingine kwa makundi mengine, au kuhukumu ufuataji wa taratibu kwa kuangalia sura ya mtu usoni

Mwisho
Kumejengeka tabia hivi sasa ya kuwamaliza wanasiasa wenye kudai uwajibikaji na uzalendo. Kumeanzishwa kiwanda kwenye medani ya siasa cha kuzalisha majungu na fitna zenye lengo la kuwachonganisha wanasiasa wa aina hiyo na wananchi kwa kutumia vyombo vya habari na nguvu ya fedha. Naamini mbinu hizi chafu, kama nyingine nyingi zilizojaribiwa kwangu huko nyuma nazo zitashindwa.

Naamini katika kweli na kweli daima huniweka huru. Naamini kuwa mwale mdogo wa mwanga wa mshumaa hufukuza kiza. Kwa imani hiyo, sitasalimu amri mbele ya dhamira zao ovu hata nitakapobaki peke yangu katika mapambano hayo ya kulinda na kutetea rasilimali za taifa zinufaishe watanzania wote.

Daima nitaongozwa na busara ya Hayati Shabaan Robert isemayo, ‘Msema kweli huchukiwa na marafiki zake, nitakapofikwa na ajali hiyo, sitaona wivu juu ya wale wawezao kudumu na marafiki zao siku zote, siwezi kuikana kweli kwa kuchelea upweke wa kitambo, nikajitenga na furaha ya kweli itakayotokea pale uwongo utakapojitenga”.

Ahsanteni sana.

Magazeti ya Leo Alhamis 2nd August 2012

ALICHOSEMA NAIBU WAZIRI KUHUSU HASARA YA AJALI YA NDEGE YA AIR TANZANIA KIGOMA.

                Hii ndio ndege pekee inayomilikiwa na Shirika la ndege ATC, moja iliyobaki ni ya kukodi.
                                      Hii ndio ndege mpya iliyokodiwa na shirika la ndege ATC.
Kwenye kipindi cha maswali na majibu Aug 1 2012 bungeni Naibu waziri wa Uchukuzi Charles Tizeba alijibu kuhusu hasara ya ajali ya ndege ya shirika la ndege Tanzania iliyotokea Kigoma tarehe 9 April 2012 pamoja na uhaba wa ndege kwa sababu shirika la ndege Tanzania linazo ndege mbili tu.

Tizeba amesema “ni kweli kwa sasa shirika la Ndege Tanzania linazo ndege mbili tu, moja ikiwa inamilikiwa na shirika lenyewe na nyingine ya kukodi, historia ya hili shirika nadhani inafahamika kwa sababu baada ya kuingia ubia wa aina mbalimbali huduma zilidorora na likaserereka kuelekea huko”


Kuhusu hasara iliyojitokeza kwenye ajali Kigoma, Naibu Tizeba amesema “ndege inayo gharama yake na ndio maana baada ya kupata ile ajali tulilipwa bima kiasi cha shilingi bilioni 10.2 lakini hasara iliyopatikana ilikua kwenye biashara hasaa na sio gharama ya ndege yenyewe.

Gharama iliyopatikana kutokana na kulazimika kuwalipia hoteli abiria walioshindwa kusafiri kutokana na ajali hiyo imetajwa kwamba ni milioni 499 ambayo ilitumika kulipia hoteli pamoja na mambo mengine.

Tayari imetangazwa na waziri wa Uchukuzi kwamba pesa hiyo ya bima itatumika kununua ndege mbili mpya.

BAADA YA MWAKA, PROFESA MWANDOSYA AINGIA BUNGENI KWA MARA YA KWANZA, ALIYOYASEMA NDIO HAYA!

Profesa Mark Mwandosya akiwa na Waziri mkuu Mizengo Pinda alipokwenda kumtembelea wakati akiumwa, hii ilikua May 7 2012.

Jumatano Aug 1 2012 nilikua nimetulia nachek bunge ghafla nikaona wabunge wanapiga meza kama kuna shangwe flani hivi, kuja kushtuka kumbe ilikua ni kutokana na waziri wa ofisi ya Rais aisekua na wizara maalum Profesa Mark Mwandosya kuingia bungeni kwa mara ya kwanza baada ya kuugua kwa zaidi ya mwaka mmoja.

Alisema “naona mkono wake mwenyezi Mungu katika uponyaji wangu, ni zaidi ya mwaka tangu nimekwenda kwa ajili ya matibabu na sijazungumza katika bunge hili tukufu, moja kati ya mambo nilikua nasema mbona ungenirudishia hata kwa dakika tano nije kuongea na wabunge wenzangu na mwenyezi Mungu ameliridhia ombi langu”

Pamoja na kuwashukuru na kuwasifu viongozi wote waliomjulia hali wa chama tawala na upinzani, Profesa Mwandosya amesema “afya ni muhimu sana na tuendelee kupima afya zetu wabunge, mimi miaka 45 sijawahi kuona kitanda hospitali nimekwenda kukikuta huko Hydrebad, nilidhani ni mtu mwenye afya sana mtu wa mazoezi kila siku asubuhi na jioni lakini kumbe mwili wa binadamu Mungu alivyoumba ni maajabu yake yeye mwenyewe”

Thanks kwa : http://millardayo.com/