Wednesday, November 21, 2012

UZINDUZI WA TUZO ZA WALIMU BORA KWA MWAKA 2012-2013



Uongozi wa Education and Expedition Agency Association kwa niaba ya kamati na bodi ya usimamizi wa tuzo hizi za walimu bora Tanzania awali ya yote tunapenda kuungana nanyi leo hii hasa kwa lengo kuu maalumu juu ya Uzinduzi wa tuzo za walimu bora Tanzania kwa mwaka 2012-2013.


Mchakato wa tuzo hizi za walimu bora Tanzania ulianza rasmi mwaka 2010 kwa kufanya tafiti takribani mikoa 18 na wilaya zake hasa kwa lengo la kutaka kujua na kufanya mazungumzo ya ana kwa ana na walimu juu ya changamoto walizo nazo.

Kila mmoja wetu hapa anatambua na hata watanzania walio wengi wanatambua  kabisa  na kuguswa na changamoto zinazowakabili walimu hapa nchini, katika kufahamu na kwa  kusikia hata sauti za walimu wenyewe.

Baada ya kukamilika kwa utafiti wetu uliofanyika kwa kipindi cha miaka (2) moja ya vitu ambavyo tuliona kuwa itakuwa ni sehemu ya msingi katika kuwapatia motisha walimu ni juu ya kuandaa tuzo hizi ambazo malengo yake makuu ni kurudisha hadhi na heshima ya walimu na kiwango cha elimu kilicho polomoka.

Walimu hapa nchini wamekuwa na mapito makubwa na changamoto nyingi za kimaisha pamoja na sehemu zao za kazi, walimu wamekuwa ni jamii ambayo haina thamani ndani ya nchi hii, sauti zao wamepaza kadri wawezavyo lakini hakuna sikio linalopokea sauti zao hata kidogo. Je tujiulize jamii hii ambayo leo haina mtu wakusikia sauti yao  madhara yake ni nini katika taifa hili hasa kwa mujibu wa kazi zao?

Hakuna taifa lolote duniani ambalo limeendelea na kupata mafanikio makubwa katika Nyanja zake zote bila msingi bora wa elimu, nasi tumegundua msingi bora wa elimu huanzia kwa mwalimu, Ikumbukwe taifa letu ni taifa changa ambalo linakabiliwa na changamoto nyingi hasa kielimu, asilimia ya watanzania wasio jua kusoma na kuandika kwa vijana na watu wazima  imekuwa ikiongezeka kwa kasi hali ambayo ni hatari kubwa sana kwa taifa letu hasa kwa mfumo tulionao wa kiulimwengu wa kuwa kijiji kimoja kutokana na ukuaji wa kitekonolojia nk.

Ikumbukwe kuwa hata kiwango cha ufauru kinachozidi kushuka kwa shule za msingi/sekondari na vyuo kila mwaka hakuna mchawi anae sababisha hali hiyo ni kutokana na  walimu kupuuzwa, kudharauliwa kuanzia kijamii chini hadi watu wa juu, mpasuko uliopo kati ya walimu na elimu inayopaswa kutolewa ni kubwa kutokana na walimu kuvunjika moyo na hali ya kujitoa katika ufundishaji? Walimu ni wazalendo thabiti sana na jamii isiyo na makuu jamii inayovumilia mapito yote, lakini bado inabeba mzigo mkubwa wa kutoa elimu katika kuifundisha jamii katika kuikoa na ujinga na kuipa maarifa stahiki  kwa mstakabali wa taifa.

Ili kurudisha na kuinua kiwango cha elimu hapa nchini msingi mkubwa hasa wa kuzingatia ni juu ya kuwajali  na kuwathamini walimu, tunaona jitihada nyingi zinaelekezwa kwenye vitu vingi katika sekta ya elimu, kama ujenzi wa vyoo, madarasa, mabweni, nk  lakini ukweli utabaki pale pale vyote unaweza kuwanavyo lakini je tujiulize vyote hivyo ni msingi wa elimu bila mwalimu. Sisi tuna amini kuwa ujenzi mzuri huanza na msingi, na katika vyote hivyo bila kujenga msingi wa walimu vyote ni sawa na bule.

Katika kutimiza adhima ya kuwa asasi ya mfano hapa nchini tumeona ni vema sasa kuelekeza nguvu ya kujenga msingi wa walimu katika kuwapa motisha ambazo tuna amini kwa nafsi moja au nyingine zitaweza kurudisha moyo na msukumo kwa walimu katika kujitoa kufundisha vizuri shuleni kwa sababu tuzo hizi ni tuzo endelevu ambazo zitakuwa zikifanyika kila baada ya mwaka, Kotokana na vigezo vya kushiriki tuzo hiyo vinalenga zaidi wajibu wa mwalimu katika kufanya kazi yake kwa usahihi basi mwalimu akiona mwalimu mwenzie amepata tuzo mwaka huu naye ataongeza juhudi na maarifa katika kazi yake ili naye apate tuzo ambayo italeta matokeo mazuri kwa wanafunzi wetu na kiwango cha elimu nchini kitapanda, kwa kutoa tuzo hiyo kwa mwanadamu wa kawaida tunaamini anaweza asiamini kuwa ndio chachu ya kurudisha hadhi, Heshima kwa mwalimu na elimu nchini lakini ni ukweli usio pingika matunda yake yataonekana hapo baade hapa nchini hasa matokeo ya utafiti tuliyo fanya.

Kwa mara ya kwanza tuzo hizi zitashirikisha walimu wa shule za msingi na walimu wa shule za sekondari kwa pande zote mbili shule za serikali na shule binafsi,pia tuzo hizi zitashirikisha walimu wa shule maalumu, na kuanzia mwaka 2015 tuzo hizi pia zitajumuisha hadi Zanzibar ili kutoa fursa kwa walimu nao kule kushiriki tuzo hizi

Kamati ya uratibu imeweza kuandaa kamati ya kutosha itakayo simamia usahili na vigezo katika kuwapata walimu bora kamati inayo ongozwa na Dr Wilson mahera Charles kutoka chuo kikuu cha dare s salaam kitivo cha hesabu (mathematics)Ambaye atashirikiana na wajumbe wengine 10 ambao ni walimu wastaafu,waratibu kutoka katika asasi za kielimu.

Vigezo vya kushiriki tuzo hizi za walimu bora tanzania

Ili mwalimu aweze kuingia na kushiriki katika shindano la utoaji wa Tuzo kwa walimu bora Tanzania, ni lazima awe na vigezo vifuatavyo;-

    Awe raia wa Tanzania
    Awe na umri kati ya miaka 18 – 54
    Awe na cheti cha kuzaliwa au cheti cha darasa la saba, au kitambulisho cha kupigia kura au pasi(passport) ya kusafiria
    Awe ameajiliwa kazi ya uwalimu kuanzia kipindi cha miaka mitano na kuendelea
    Awe na mahudhurio mazuri kazini na kuhudhuria vipindi vyote vya kufundisha darasani
    Awe ni mtu wa kujitoa kwa ajili ya maendeleo ya elimu nchini
    Awe muadilifu kazini na katika jamii anayoishi
    Awe anayejua wajibu wa kutimiza malengo ya kazi yake kwa kuandaa;-

           (i)Azimio la kazi (ii)Andalio la somo  (iii)Andalio la notes

     9.  Awe na  Haiba inayo jitosheleza

    10.  Awe na Ushirikiano mzuri kati yake na walimu wenzie na wanafunzi kwa ujumla

    11.  Awe na uwezo wa kutosha katika kushauri walimu, wanafunzi, viongozi na jamii kwa ujumla

    12.  Awe mbunifu na anayemudu kukabiliana na changamoto zilizopo mfano;-mazingira duni ya kazi yake nk.

    13.  Asiwe na tuhuma za rushwa au aliye wahi kuwa na kosa la jinai

    14.  Awe anavaa uasilia kwa vitendo

    15.  Awe na matokeo mazuri kwa wanafunzi kwa ngazi zote anazo fundisha

    16.  Awe ameajiriwa na serikali au sekta binafsi

    17.  Awe tayari kushiriki mambo ya jamii mfano;- michezo,mazingira,majanga, nk.

    18.  Awe anaendana na sera ya elimu

    19.  Awe anaye kubalika na wafanyakazi wenzie na hata wanafunzi kwa ujumla

    20.   Asiwe amecha kazi ya uwalimu na kurudia kazi ya uwalimu

    21.  Awe amesomea taaluma ya uwalimu katika chuo/vyuo vinavyotambulika kiserikali.

Mchakato utakavyo endeshwa katika kuwapata washindi

Tutaanza kufanya mchakato wa kusambaza fomu za washiriki mikoa yote hapa nchini hadi wilayani na fomu hizo zitapatikana kupitia matawi yote ya benki ya posta Tanzania wakiwa ni miongoni mwa wafadhili wa tuzo hizi. sababu zilizopelekea fomu kutokwenda sawa na uzinduzi huu ni kutokana na kuchelewa kukamilika kwa taratibu zilizo jitokeza nje ya uwezo wetu.

fomu hizo zitaanza kupatikana rasmi kuanzia Desenba 15/2012 hadi februari 10/2013 na ndio utakuwa mwisho wa kuchukua fomu. jinsi ya kuwahamisisha walimu kujitokeza kuchukua fomu hizo tumeandaa matangazo yatakayokuwa yakitolewa na vyombo vya habari hapa nchini hususani ITV na Redio ONE ambao ni wafadhili  wetu.

Baada ya walimu kuwa wamekamilisha zoezi la kuchukua fomu hatua itakayo fuata walimu watatangaziwa tarehe za usahili kila mkoa kupitia vyombo vya habari.

Baada ya usahili matukio yote ya uendeshaji wa tuzo hizi ikiwa ni pamoja na kuanzia ngazi za mikoa, ngazi ya kanda hadi ngazi ya Taifa yote yatakuwa yakiratibiwa kupitia kipindi maalumu kitakacho itwa ni wakati wa mwalimu kupitia ITV hadi siku ya kilele cha utoaji wa tuzo hizo Tarehe 25/11/2013.

Ndani ya mchakato huo utakavyo kuwa unaendelea pia tutatoa fursa kwa wananchini kushiriki kutoa maoni ya mwalimu mulengwa ambaye wanaishi naye karibu na kupiga kura kupitia namba maalumu ya simu za mkononi itakayo tangazwa hapo baadae ikiwa ni pamoja na fursa ya watu kutoa maoni kupitia tovuti yetu na mitandao ya kijamii.

Zawadi za washindi watakao shinda tuzo hizi ni kama ifuatavyo-:

A- washindi katika makundi 2 upande wa s/msingi na sekondari ni kama ifuatavyo?

mshindi 1- milioni 40 taslimu, pamoja na ufadhili wa kusoma kwa mwaka million 5 kwa miaka mitatu milioni 15. Jumla kuu million 55

Mshindi wa 2- million 30 taslimu, pamoja na ufadhili wa kusoma kwa mwaka million 4 kwa miaka 3 jumla million 12. Jumla kuu million 42.

Mshindi  wa 3 – million 20 taslimu, pamoja na ufadhili wa kusoma kwa mwaka million 3 kwa miaka 3 jumla million 9. Jumla kuu million 29

Mshindi wa 4 – million 10 taslimu, pamoja na ufadhili wa kusoma kwa mwaka million 2 kwa miaka 3 jumla million 6.  Jumla kuu million 16

Mshindi wa 5 – million 5 taslimu, pamoja na ufadhili wa kusoma kwa mwaka  milion  2 kwa miaka 3 jumla million 6. Jumla kuu million 11

washindi wa sita hadi 10 kila upande watapata pikipiki mojamoja zenye thamani ya milioni 2,na laptop yenye thamani ya milioni 1.5 jumla milioni 3,500,000/= kila mmoja atapata zawadi yenye thamani ya 3,500,000/=

Washindi wa masomo kila somo moja watakuwa washindi 10 s/msingi  washindi kumi 10 s/sekondari na jumla ya somo moja lina washindi 20 na mosomo yapo sita jumla watakuwa washindi 120, ambao watapata zawadi ya Tshs laki 3 na baiskeli 1 yenye thamani ya laki mbili kwa kila mshindi.

Na masomo hayo yatakayo shindaniwa ni kama itutavyo-:

1.        Sayansi

2.        Hisabati

3.        kiswahili

4.        Geograph

5.        Historia

6.        English

Ifuatayo ni taarifa ya Harambee ya kuchangia Mchakato wa Tuzo za walimu bora uliofanyika tarehe 2 november 2012 katika ukumbi wa Diamond jubilee V.I.P.

Siku ya harambee tulifanikia kupata kiasi cha sh. 42,000,000/= na ahadi walizotoa wananchi ni kiasi cha sh. 143,000,000/=  na bado tunaendelea kupokea ahadi na kufuatilia ahadi zilizotolewa siku ya harambee

Na mwisho kabisa tunapenda kutoa ombi kwa wafadhili wengine waweze kujitokeza zaidi katika kufadhili tuzo hizi ili tuweze kutoa zawadi kwa walimu wengi zaidi.

Waandishi wa habari na vyombo vyote vya habari  tunapenda kutoa ombi letu kwenu katika kuzitangaza vema tuzo hizi.

Pia na chukua fursa hii kuwashukuru wafadhili waliojitokeza Benki ya posta Tanzania, ITV na Redio one Vio company ltd,wise company limited,ipo professional ltd,na wote walioshiriki kuchangia kwa namna moja au nyingine tuzo hizi za walimu bora tanzanania.

Ahsanteni

Clemence A.Kambengwa

M/kiti EEAA 

Magazeti ya leo Jumatano 21rd November 2012

MATOKEO YA MECHI ZOTE ZA UEFA NOV 20 NA MAJINA YA WAFUNGAJI WAKE.

SABABU ZA ZITTO KABWE KUANDIKA KWAMBA “TUSIGEUZWE MAZEZETA, MABWEGE NA MAZEZETA HUIMBA KILA WANACHOAMBIWA”

Mabilioni ya Uswisi – Tusigeuzwe Mazezeta

Jumanne tarehe 20 Novemba 2012, baadhi ya vyombo vya habari vimebeba habari zinazohusu matamshi ya Waziri wa Utawala Bora ndugu George Mkuchika kuhusu sakata ya mabilioni ya Uswisi. Waziri amesema kwamba Serikali ya Uswisi inataka majina ya Watanzania walioficha fedha huko ndio waweze kusaidia uchunguzi. Habari kama Hiyo, yenye maudhui na malengo hayo hayo iliandikwa na Gazeti la The Guardian on Sunday la tarehe 18 Novemba 2012.

Nimeona ni vema nitoe kauli yangu rasmi kuhusu suala hili. Lengo ni kuweka rekodi sawa juu ya Azimio la Bunge na kwamba Serikali inapaswa kutekeleza Azimio na sio kutoa kauli tata za kukata tamaa.

Moja, Suala hili japo sio jipya lakini limeandikwa kama ni jambo jipya. Suala la Serikali ya Uswisi kutaka majina lilisemwa na Mwanasheria Mkuu wa Serikali wakati akichangia hoja binafsi niliyowasilisha Bungeni na pia wakati akileta maombi yake ya kuiondoa hoja ambayo yalikataliwa na Bunge. Kama sio sababu mpya ni kwanini imeibuka upya na kwa kasi? Ni wazi Serikali inajihami kwa kuona kuwa itashindwa kutekeleza azimio la Bunge. Watanzania wasikubali propaganda hii ya Serikali. Bunge limeagiza Serikali kufanya uchunguzi kwa kutumia njia za kiserikali au wachunguzi binafsi wa kimataifa.

Kwa nini Serikali inaanza kubwabwaja ilhali wala haijaanza kazi hiyo? Serikali inajaribu kuficha nini? Kwa nini baada ya wiki iliyopita Benki Kuu kufanya uchunguzi kwenye Mabenki ya Biashara jijini Dar es Salaam na namna fedha zimekuwa zikipelekwa nje (international transfers), leo Serikali inakuja na kauli za kukakata tamaa? Kunani?

Pili, Watanzania wajue kwamba Taifa la Swiss limejengwa na linajengwa kwa fedha hizi za wizi ambazo watu mbalimbali duniani wanaiba au kukwepa kodi kwenye nchi zao na kuzificha huko. Serikali ya Swiss hata siku moja haiwezi kutoa ushirikiano kwa Serikali ya Tanzania katika suala kama hili. Ndio maana Azimio la Bunge linataka wachunguzi binafsi ambao hawatahitaji ushirikiano wa Serikali ya Swiss.

Nawakumbusha kwamba mwaka 1997 mara baada ya Joseph Desire Mobutu kuangushwa na Rais Joseph Kabila kule Kongo – Kinshasa, Serikali ya Swiss iliitaka Serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo kuonyesha ushahidi kuwa hela hizo za Mobutu zilikuwa zimepatikana kwa njia haramu! Waswiss walitaka Kabila awakakikishie kuwa fedha zile zaidi ya dola bilioni nane za Kimarekani Mobutu hakuzipata kihalali ndio waweze kuzirejesha. Zaire ilikadiriwa kuwa na zaidi ya dola za Kimarekani bilioni thelathini katika Mabenki ya nje ya nchi hiyo. Majibu ya aina aina hii ni majibu ‘standard’ ambayo kila nchi inapewa.

Hata Marekani ilipokuwa inafuatilia wakwepa kodi wao walijibiwa hivi hivi. Hatimaye Serikali ya Marekani ikaamua kununua taarifa hizo na kuwakamata wakwepaji kodi wao walioficha fedha Uswisi. Hao ndio Waswiss ambao Serikali ya Tanzania inashabikia majibu yao. Bila Aibu Mawaziri wetu wanayanukuu majibu ya Waswiss kama kasuku. Tunasahau historia haraka sana. Tunakuwa kama mazezeta.

Tusiwe Taifa la mazezeta. Mabwege na mazezeta huimba kila wanachoambiwa kuimba. Sasa Serikali ya Tanzania imekuwa msemaji wa Serikali ya Swiss badala ya kuchunguza utoroshaji wa fedha haramu na kisha kutoa taarifa Bungeni. Naitaka Serikali ianze uchunguzi mara moja kama namna ilivyoelekezwa na Bunge. Suala hili sio suala la kisiasa, sasa ni Azimio la Bunge ambalo linahitaji kutekelezwa kikamilifu. Suala hili sio suala la Zitto Kabwe tena, ni suala la Bunge, ni suala la Wananchi. Wananchi hawataki uzezeta wa watu waliopewa dhamana ya kutekeleza Azimio lao.

Kama hawawezi wapishe watu wenye uwezo wa kusimamia maslahi ya Watanzania kwa kuchukua hatua stahili za kuchunguza utoroshaji mkubwa wa fedha za kigeni, ukwepaji mkubwa wa kodi na ufisadi uliopelekea Watanzania kuficha mabilioni kwenye mabenki nje ya Tanzania. Hatutakaa kimya mpaka tuone mwisho kamilifu wa suala hili. Utekelezaji wa Azimio la Bunge itakuwa ni salamu tosha mafisadi na watoroshaji wa fedha haramu kwamba hawana pa kujificha na Tanzania sio Taifa la kuchezeachezea. Lazima tushinde vita hii. Anayeona hawezi kutuongoza kuishinda atupishe mapema. Hatupaswi kuwa Taifa la Mazezeta. Watanzania sio mabwege tena, Mwakyembe alipata kusema.

Kabwe Zuberi Zitto, Mb

Kigoma Kaskazini.