Monday, July 30, 2012

CCM,Chadema Wawatangazia Kiama Wabunge Mafisadi

DK SLAA AONYA HAKUNA HURUMA, MSEKWA ASEMA RUSHWA ADUI WA HAKI, MBATIA ATOA WIKI MOJA SPIKA AWATAJE WOTE

VYAMA vya CCM na Chadema vimetoa onyo kali kwa wabunge wanaotuhumiwa kwa kashfa ya kuhongwa na baadhi ya kampuni za mafuta na kulihujumu Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco), vikisema havitasita kuwawajibisha pindi tuhuma hizo zitakapothibitika.

Kauli ya vyama hivyo imekuja siku moja baada ya wabunge watano, watatu wa CCM na wawili wa upinzani kudaiwa kuhusika na vitendo hivyo vya rushwa, ambavyo vimesababisha Spika wa Bunge, Anne Makinda kuivunja Kamati ya Bunge ya Nishati na Madini na kuagiza uchunguzi wa kina ufanyike ili majina ya wahusika yawekwe hadharani.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti jana, viongozi wa juu wa vyama hivyo walisema wanasubiri kwa hamu taarifa rasmi kutoka bungeni.

CCM: Rushwa adui wa haki
Makamu Mwenyekiti wa CCM Bara, Pius Msekwa alisema chama hicho kimewaapiza wanachama wake wote kutotoa wala kupokea rushwa.

Alisema rushwa ni kosa la jinai hivyo anaamini vyombo husika vya dola vitachukua hatua zinazofaa kwa mujibu wa sheria za nchi.

Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye alikazia kauli hiyo akisema rushwa inaelezwa katika katiba ya chama hicho kwamba ni, ‘adui wa haki’ na wanachama wote waliapishwa kuwa hawatapokea wala kutoa rushwa.
Alisema yeyote anayekwenda kinyume na kanuni za CCM, anajiweka katika kundi la wasaliti wa chama.

Alisema wabunge ni kundi maalumu nchini ambalo linalipwa vizuri ili lisimamie vyema misingi ya maendeleo ya nchi pasipo tamaa wala vishawishi hivyo wanapotajwa miongoni mwa kundi la wala rushwa, CCM kinalaani vikali tukio hilo.

Kuhusu tuhuma hizo kutajwa kuwahusisha wabunge watatu wa chama hicho, Nape aligoma akisema habari hizo siyo rasmi, hivyo hawezi kuzizungumzia.

Hata hivyo, alisema CCM kinasubiri uchunguzi ufanyike ambao ndiyo utakaoweka bayana wahusika wa tuhuma... “Tusubiri uchunguzi ukamilike. Idadi inawezekana ikawa hiyo au ikapungua au kuongezeka.”

Dk Slaa: Hatufumbii macho ufisadi
Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa alisema: “Nalaani kitendo cha wabunge kuhusishwa na ufisadi hasa ikizingatiwa kwamba Chadema tumekuwa tukiupinga vikali. Tumekuwa tukipinga rushwa kwa sababu ndiyo inayoielekeza nchi pabaya… Chadema hatufumbii macho rushwa.”

Alisema tangu kuanza Bunge la 10, Chadema kimekuwa kikiona baadhi ya mambo yanayoendelea katika mhimili huo muhimu wa dola yamejaa walakini... “Ndiyo maana sisi Chadema tumekuwa tukisema Bunge limepoteza mwelekeo.”

Alisema akiwa mtendaji mkuu wa chama, anasubiri taarifa kamili kutoka katika kikao cha wabunge wa chama hicho ili kuweka wazi majina ya wahusika na kisha kufuatiwa na kikao cha Kamati Kuu (CC) ambacho kitakaa na kuchukua hatua kali.

“Tunahitaji tupate maelezo ya kina... chama chetu hakikurupuki… Nasubiri taarifa ya kokasi ya chama. Katiba ya Chadema inatambua uwapo wa kikao cha wabunge wetu na kwa bahati nzuri, kiongozi wake mkuu ni Mwenyekiti wa Chadema (Freeman Mbowe) na katibu (David) Silinde ni mbunge wetu. Tunasubiri taarifa yao.”

Alisema Chadema kina kanuni ya kudhibiti rushwa hivyo, mbunge wake akitajwa miongoni mwa wanaohusishwa na rushwa, atawajibishwa kupitia kikao cha CC ya chama hicho.

NCCR-Mageuzi yakoleza moto

Katika hatua nyingine, Chama cha NCCR- Mageuzi jana kilikoleza moto baada ya kumtaka Spika Anne Makinda awataje wabunge hao bungeni ili wafukuzwe na kufungwa kama Sheria ya Haki, Kinga na Madaraka ya Bunge inavyotaka.
  Chanzo:  http://www.mwananchi.co.tz

No comments: