Monday, July 2, 2012

MAMA ULIMBOKA: NAMWACHIA MUNGU


KUFUATIA tukio la mwanaye ‘kusulubiwa’ wiki iliyopita, mama mzazi wa Dk. Steven Ulimboka ambaye hakutaka jina lake lipambe ukurasa huu, ameliambia Ijumaa Wikienda kuwa anashukuru Mungu kwa kwenda kumuona mtoto wake na kumkuta akiwa hai.

Baada ya kumuona mwanaye akipatiwa matibabu kwenye Taasisi ya Mifupa Moi katika Hospitali ya Muhimbili, Dar, mama huyo alisema tatizo lililompata mwanaye anamwachia Mungu kwani ndiye mwamuzi wa uhai wa kila mtu hapa duniani.

“Namwambia Mungu asante kwa kuwa nimemkuta yupo hai. Kwa jinsi nilivyopata taarifa niliamini mwanangu amefariki dunia japo hali yake si ya kuridhisha,” alisema kwa uchungu.
Jumamosi mchana, Dk. Ulimboka alisafirishwa kupelekwa Afrika Kusini kwa ajili ya matibabu kufuatia kubainika kuwa ubongo wake ulikuwa umetikisika.

Dk. Ulimboka alitekwa na watu wasiojulikana usiku wa kuamkia Jumatano wiki iliyopita katika Viwanja vya Leaders Club, Kinondoni ambapo alipigwa vibaya na kwenda kutupwa kwenye msitu wa Pande nje kidogo ya jiji.

Tukio hilo limekuwa ndiyo habari ya mjini kwa sasa kwani lilitokea katika kipindi ambacho madaktari wapo kwenye mgomo huku Dk. Ulimboka akiwa ndiye kiongozi wa jumuiya yao.

No comments: