Tuesday, May 14, 2013

WENYE MABASI WATAKA NAULI IPANDE TENA

BAADHI ya wamiliki wa mabasi mkoani Shinyanga, wamesema asilimia 24.46 iliyoongezwa katika nauli haitoshi.

Wamiliki hao wameyasema hayo ikiwa ni takriban mwezi mmoja tangu kuanza kutumika kwa nauli mpya za usafiri wa barabara, reli na kupandishwa kwa tozo za huduma za meli bandarini. Hatua hiyo ilichukuliwa na Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri wa Nchi Kavu na Majini (SUMATRA), Aprili 3 mwaka huu.

Wakizungumza na Mtanzania kwa nyakati tofauti mjini Shinyanga, baadhi ya wamiliki wa mabasi na wadau wa sekta ya usafirishaji nchi kavu, walisema awali wao waliwasilisha mapendekezo yao kwa SUMATRA wakiomba kupandishwa kwa nauli kwa asilimia 149.

Mmoja wa wamiliki wa mabasi ambaye hakuwa tayari kutajwa jina lake , alisema kutokana na kupanda kwa bei ya spea za magari na gharama za uendeshaji, kampuni nyingi kwa sasa zinashindwa kufanya matengenezo ya mabasi yao.

Alisema katika mwaka mmoja uliopita, tairi ya gari kubwa ilikuwa ikiuzwa Sh 400,000 lakini kwa sasa inauzwa Sh 650,000. Wakati huo bima ilikuwa Sh 450,000 lakini sasa imepanda hadi Sh 1,000,000, alisema.

Alitaja gharama nyingine kuwa ni kodi zinazotozwa na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), ushuru wa kituo cha mabasi Sh 2,000 na ada ya Chama cha Madereva Sh 5,000 ambazo hutozwa kwa kila basi linaloingia katika kituo cha mabasi.

No comments: