Tuesday, July 3, 2012

DAKTARI MWINGINE ATEKWA

WAKATI Kiongozi wa Chama Cha Madaktari nchini Dk. Steven Ulimboka akiwa amesafirishwa kwenda Afrika Kusini kwa matibabu, Daktari mwingine, John Chilinde ametekwa na kupigwa ambapo amejeruhiwa sehemu mbalimbali za mwili wake.

Daktari huyo ambaye ni mkazi wa Tabata Kimanga , wilayani Ilala anayetibu katika Hopitali ya Mwananyamala jijini Dar es Salaam alitekwa Ijumaa saa tano usiku akiwa anatoka baa iitwayo Flora Pub iliyopi Tabata jijini.

Habari zinasema akiwa anatoka katika baa hiyo, Dk Chilende alitekwa na vijana watatu ambao walimshambulia huku wakimuuliza kwa nini wamegoma kutibu watu katika hospitali za serikali.
Taarifa zaidi zinaeleza kuwa Dk. Chilende alishambuliwa kwa dakika kumi na baadaye kutekwa kisha akaenda kutelekezwa akiwa hoi hajitambui hatua chache kutoka sehemu aliyokuwa anapigiwa .

Chanzo kimesema daktari huyo aliokolewa na dereva wa kibajaji ambaye alimkuta akigagaa chini huku akivuja damu mdomoni, alimpakia na kumpeleka Kituo cha Polisi Buguruni ambako alifunguliwa jalada namba BUG/RB/7974/ 2012 (Shambulio la kudhuru mwili), baadaye alikimbizwa katika Hospitali ya Amana kwa matibabu zaidi.

Afisa mmoja wa polisi wa Kituo cha Buguruni ambaye hakupenda jina lake kuandikwa gazetini kwa kuwa siyo msemaji, alithibitisha kutokea kwa tukio hilo na akaongeza kuwa wahusika wa unyama huo wanasakwa kwani daktari huyo anamfahamu mmoja wa waliyemshambulia. Kamanda wa Kanda Maalum, Suleiman Kova hakupatikana kuzungumzia tukio hilo. Chanzo: Globalbuplisher

No comments: