Thursday, May 2, 2013

WABUNGE WATWANGANA NGUMI NDANI YA BUNGE...

                                                               Bunge la Venezuela.
Makonde yameibuka bungeni na baadhi ya wabunge kujeruhiwa katika sintofahamu, kutokana na mjadala kuhusu uchaguzi wa hivi karibuni unaobishaniwa.

Upande wa upinzani ulisema juzi kwamba wabunge wao saba, walishambuliwa na kujeruhiwa wakati wakipinga hatua ya kuwazuia kuzungumza katika Bunge hilo, kutokana na kukataa kwao kutambua ushindi wa Rais Nicolas Maduro uliofanyika Aprili 14.

Wabunge wa chama tawala walilaumu wapinzani wao hao na kuwaita mafashisti kwa kuanzisha vurugu, hali iliyoonesha siasa tete katika Taifa hili mwanachama wa OPEC baada ya kifo cha Msoshalisti, Hugo Chavez mwezi jana.


“Tulijua wapinzani wamekuja hapa kuanzisha ghasia,” Maduro alisema kutokana na tukio hilo. “Hii haipaswi kujirudia.”
Maduro (50), ambaye aliteuliwa na Chavez kuwa mrithi wake, alimshinda mgombea wa upinzani Henrique Capriles kwa asilimia 1.5 za alama.
Capriles (40) amekataa kutambua ushindi wake, akidai kuwapo kwa idadi kubwa ya upungufu na kwamba kura ziliibwa.
Uchaguzi huo ulibainisha mgawanyiko dhahiri wa Taifa hili baada ya miaka 14 ya utawala wa kisoshalisti wa Chavez.

“Wanaweza kutupiga, kutufunga, kutuua, lakini hatutaweza kukiuka kanuni zetu,” mmoja wa wabunge wa upinzani, Julio Borges, alikiambia kituo cha televisheni, akionesha uso wenye michubuko na damu. “Masumbwi haya yanatuongeza nguvu,” alisema.

Mfanyakazi wa Bunge, ambaye aliomba asitajwe jina, alisema tatizo lilianza pale wabunge wa upinzani, walipopiga kelele za “fashisti” dhidi ya kiongozi wa Bunge na kufunua bango la kupinga lenye maandishi ya “mapinduzi ya Bunge”.

Wabunge wa chama tawala waliwashambulia. Kompyuta mpakato na meza, vilitumiwa kushambuliana, huku mbunge mmoja akipigwa kichwani na kiti, shuhuda alisema.

Baadaye wafanyakazi walilazimishwa kuonesha simu zao, kama zilikuwa na picha au video kuhusu tukio hilo, mfanyakazi wa Bunge aliongeza.

Mbunge wa chama tawala, Odalis Monzon, alisema yeye na wenzake walishambuliwa na kupigwa. “Leo tena nililazimika kulinda urithi wa kamanda (Chavez),” alisema.

Vurugu hizo zilianza baada ya Bunge hilo linalodhibitiwa na serikali, kupitisha hatua inayonyima upinzani haki ya kuzungumza bungeni hadi umtambue Maduro kama rais.

“Mpaka watambue mamlaka, taasisi za Jamhuri, uamuzi wa watu wetu, wabunge wa upinzani waende wakazungumze na vyombo vya habari vya binafsi na si hapa bungeni,” alisema Diosdado Cabello, ambaye ni Spika wa Bunge.

Pande zote mbili zilianza kushutumiana faragha bila waandishi wa habari kuwapo. Video zilizopatikana na kituo cha televisheni chenye ufuasi wa upinzani cha Globovision kutoka kwa mmoja wa wabunge, zilionesha wabunge hao wakipigana huku wengine wakipaza sauti za kuwazuia.

Venezuela imekuwa katika mgogoro tangu uchaguzi wa Aprili 14. Takribani watu wanane walikufa katika maandamano siku mmoja baada ya uchaguzi. Kumekuwa na kamatakamata ambayo wapinzani wanaiita wimbi la ukandamizaji.

Maduro ametuhumu upinzani kwa kupanga mapinduzi. Mtawala wa zamani wa Taifa hili, Hispania, wiki hii alitoa mwito wa kufanyika mazungumzo ya kuondoa mvutano wa kisiasa nchini. Lakini, Maduro alikataa.

“Acheni kuingiza pua zenu Venezuela. Waziri wa Mambo ya Nje wa Hispania, ondoka, wewe fidhuli. Venezuela lazima iheshimiwe,” alisema Maduro katika hotuba yake akimaanisha Waziri wa Mambo ya Nje, Jose Manuel Garcia-Margallo.

No comments: