Monday, April 15, 2013

MAJID MJENGWA NAYE AKAMATWA NA POLISI AKIHUSISHWA NA SAKATA LA KIBANDA

                                                                        Majid Mjengwa.
  MWANDISHI wa safu katika magazeti mbalimbali nchini, Majid Mjengwa amekamatwa na polisi kwa tuhuma za kuhusika na tukio la kushambuliwa kwa Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), Absalom Kibanda.

Habari zilizoufikia mtandao huu jana mchana na baadaye kuthibitishwa na polisi zinasema Mjengwa alikamatwa muda wa asubuhi na kwamba alikuwa akihojiwa na makachero wa jeshi hilo hadi alasiri kuhusu tukio la kuteswa kwa Kibanda.

Msemaji Mkuu wa Polisi Advera Senso alisema kwamba:

“Ni kweli kwamba tunaye, tunaendelea kumhoji, tunachoomba ni kwamba mtupe nafasi ili tufanye kazi yetu na kukiwa na jambo lolote tutawajulisha.”

Hata hivyo, Senso hakuwa tayari kueleza kwa undani muda aliokamatwa Mjengwa wala sababu za kukamatwa na kuhojiwa kwake, lakini chanzo chetu ndani ya Jeshi la Polisi kilithibitisha kwamba pamoja na mambo mengine kuhojiwa kwake kulihusu uteswaji wa Kibanda.

Jumatatu wiki hii, Kaimu Mkurugenzi wa Makosa ya Jinai Nchini, Issaya Mngulu alisikika akizungumza na Kituo cha Radio One cha Dar es Salaam kwamba kesho Jumatatu (April 15, 2013) polisi watatoa taarifa rasmi ya hatua waliofikia katika upepelezi wa kesi ya Kibanda.

Kwa upande wake Mia Mjengwa ambaye ni mke wa Mjengwa, alisema mumewe alipata wito kutoka polisi makao makuu Alhamisi na kwamba juzi Ijumaa alisafiri kutoka Iringa kwenda Dar es Salaam kuitikia wito huo.

“Ninachojua ni kwamba aliitwa kwenda polisi na leo (jana) alinipigia simu kama saa 7:00 mchana na aliniarifu kwamba yupo polisi, sasa tangu wakati huo sijaongea naye tena na wala simu zake hazipatikani,” alisema Mia na kuongeza: “Kwa hiyo mimi kwa kweli sifahamu kwamba anahojiwa kwa sababu gani.”

Taarifa za kukamatwa kisha kuhojiwa kwa Mjengwa ambaye pia ni mmiliki wa Mjengwa Blog, zimekuja siku chache tangu msaidizi wake katika Blog hiyo, Joseph Ludovick akamatwe, kuhojiwa kisha kufikishwa mahakamani kwa tuhuma za ugaidi.

Ludovick alifikishwa mahakamani pamoja na Mkurugenzi wa Usalama wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Willifred Lwakatare wakikabiliwa na tuhuma za ugaidi na kupanga kumteka Mhariri Mtendaji wa Mwananchi, Dennis Msacky.

Kuteswa Kibanda.
Machi 5, mwaka huu saa 5.30 usiku, Kibanda ambaye pia ni Mhariri Mtendaji wa Magazeti ya Kampuni ya New Habari (2006) Ltd, alinusurika kifo baada ya kuvamiwa na watu wasiojulikana nyumbani kwake kisha kupigwa na kujeruhiwa vibaya.

No comments: