Saturday, July 7, 2012

DILMA ROUSSEF: MWANAMKE WA KWANZA KUWA RAIS BRAZIL

                                                                  Dilma Vana Roussef.
UKWELI ni kwamba mamilioni ya watu duniani wanaifahamu nchi ya Brazil, hususan kutokana na umaarufu wake katika soka. Lakini ni wachache wanaowafahamu marais waliowahi kushika madaraka katika nchi hiyo kwa miaka nenda rudi.

Aidha, ni watu wachache wapenzi wa nchi hiyo ya Kusini mwa Bara la Amerika na ya tano kwa ukubwa wa eneo duniani ikiwa na watu milioni 192, wanafahamu kwamba rais wake wa sasa ni mwanamke.

Ni Dilma Roussef, mama mwenye wajihi na umbo la kuvutia kwa wanaume na wanawake licha ya kuwa na umri wa miaka 64 sasa.

Roussef ambaye majina yake kamili ni Dilma Vana Roussef, aliweka rekodi katika nchi hiyo kwa kuwa mchumi (economist) wa kwanza kushika nafasi hiyo nchini Brazil.

Dilma, aliyezaliwa Desemba 14, 1947 nchini Brazil na akashika wadhifa wa urais Januari 1, 2011, ni rais wa 36 wa nchi hiyo ambayo ilianza kujulikana hivyo mwaka 1500 baada ya Wareno kutoka Ulaya (Portugal) wakiongozwa na Pedro Álvares Cabral kufika huko na kulifanya eneo hilo kuwa koloni.

Rais Roussef ambaye ana mtoto mmoja wa kike aitwaye Paula aliyempata akiwa na mwanasiasa mwenzake, Carlos Araujo, alifanya kazi chini ya Rais Mstaafu, Luiz de Silva (aliyemrithi) akiwa msaidizi mkuu wake (Chief of Staff) ambapo alikuwa ni mtu wa pili mwenye mamlaka zaidi nchini humo.

Vilevile, Dilma, msomi wa Chuo Kikuu cha Shirikisho cha Rio de Grande dol Sul, aliyewahi kuwa waziri wa madini na nishati na aliupata urais huo kupitia Chama cha Wafanyakazi, katika harakati za siasa aliwahi kufungwa 1970 hadi 1972 na kuteswa wakati wa kupinga utawala wa kijeshi nchini humo.

Ni Dilma Roussef, binti wa baba mwenye asili ya Bulgaria ambaye alimwoa mwanamke wa Kibrazil baada ya kukimbia machafuko Ulaya wakati wa Vita Kuu ya Pili ya Dunia na kwenda kuishi Brazil.

No comments: