Tuesday, July 31, 2012

Wabunge Wazidi Kuongezewa Marupurupu

MARUPURUPU ya wabunge ikiwamo mishahara imeongezwa kutoka Sh7.4 milioni kwa mwezi hadi takriban Sh11milioni kwa mwezi, hatua ambayo imeibua mjadala mwingine mzito miongoni mwao.

Tangu mwaka jana, wabunge wamekuwa katika vita ya kupokea au kutopokea posho ya vikao ambayo imekuwa ikikolezwa na Mbunge wa Kigoma Kaskazini (Chadema), Zitto Kabwe ambaye alizikataa akisema mbunge anapokuwa kazini hahitaji kulipwa.

Hata hivyo, uchunguzi wa gazeti hili umebaini kwamba sasa vita kubwa ipo katika marupurupu mapya ambayo pamoja na kuchanganya na mshahara yanafikia Sh11milioni kwa mwezi.

Spika wa Bunge, Anne Makinda alipoulizwa jana alithibitisha kuhusu kuongezeka kwa malipo jumla ya wabunge kwa mwezi lakini akasema hafahamu kiwango halisi kilichoongezwa.

Makinda alisema nyongeza iliyopo siyo kwa wabunge tu, bali watumishi wote wa Serikali na ilitangazwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (Menejimenti ya Utumishi wa Umma), wakati wa Bajeti ya Ofisi hiyo kwa mwaka 2012/13.

“Hiyo nyongeza siyo tu kwa wabunge, bali ni kwa watumishi wa Serikali. Tena hiyo ilitangazwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (Menejimenti ya Utumishi wa Umma). Sasa ukiniuliza kiasi gani hapo ndipo sielewei, ila najua nyongeza ipo,” alisema Spika.

Lakini, vyanzo kutoka ndani ya Bunge vilisema kwamba nyongeza hiyo ambayo tayari imeingia katika mshahara wa Julai ni Sh3.6milioni, hivyo kufanya jumla ya fedha anazochukua mbunge kufikia kiasi hicho cha Sh11milioni.
“Hiyo ni vita, kuna wabunge wana hasira kweli hawataki wananchi wajue kama marupurupu yameongezeka.

Wanaona wananchi wakijua itakuwa ni tatizo kubwa, watapigiwa kelele lakini nyongeza hiyo ipo. Tayari wengine wamechukua tangu Ijumaa,” kilisema chanzo kimoja kwa sharti la kutotajwa jina gazetini.

Hata hivyo, kwa mujibu wa chanzo hicho, baadhi ya wabunge kutoka kundi la wanaopinga posho kwa wabunge wamepinga pia nyongeza hiyo wakitaka fedha hizo zielekezwe katika sekta nyingine za kijamii.

Marupuru ya sasa
Hadi mwezi uliopita, mbunge alikuwa akipokea Sh7.4milioni kwa mwezi ambazo kati ya hizo Sh2.5milioni ni kwa ajili ya mafuta, Sh2.3 mshahara, Sh170,000 kwa ajili ya mshahara wa dereva, 100,000 kwa ajili ya katibu wa mbunge na posho ya jimbo.

Hata hivyo, katika nyongeza hiyo ya sasa haijawekwa wazi kwamba kiasi gani ni kwa ajili ya mshahara, fedha za mafuta ya gari la mbunge, za dereva, katibu na za posho ya jimbo na tayari baadhi ya wabunge wameanza kufuatilia mchanganuo wa nyongeza hiyo.

Chanzo:
http://www.mwananchi.co.tz/habari

No comments: