Tuesday, July 31, 2012

Tamko La Chadema Kuhusu Kufungiwa Kwa Gazeti La Mwanahalisi


TAMKO LA CHAMA CHA DEMOKRASIA NA MAENDELEO (CHADEMA)

KUHUSU KUFUNGIWA KWA MWANAHALISI

Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kinalaani uamuzi wa Serikali inayoongozwa na Chama Cha Mapinduzi (CCM) kulifungia kwa muda usiojulikana gazeti la MwanaHalisi kwa kutumia mwanya wa sheria mbovu ya magazeti inayokwenda kinyume na haki za binadamu na utawala bora.

CHADEMA kinaitaka Serikali kulifungulia gazeti hilo haraka iwekanavyo na kimewasiliana na Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inayoongozwa na CHADEMA kuchukua hatua za kibunge kuisimamia Serikali kurekebisha udhaifu huo ikiwa inaheshimu uhuru wa habari na inazingatia maslahi ya taifa.

CHADEMA kinatafsiri hatua hiyo ya Serikali ya kufungia gazeti la MwanaHalisi kuwa ni sawa na kufungia uhuru wa kusambaza habari, uhuru wa kupokea habari na uhuru wa kutoa maoni, hivyo tunatoa mwito kwa wananchi na wadau wote wa habari kuungana pamoja kupinga hatua hiyo, na CHADEMA kitaeleza hatua za ziada za kuchukuliwa iwapo Serikali haitasikiliza kauli za wadau wa habari juu ya suala hili.

CHADEMA kinatambua kuwa uamuzi wa Serikali kufungia gazeti hilo kwa mara nyingine tena ni kwenda kinyume na haki za binadamu, kinyume na utawala bora na ni kikwazo kwa demokrasia na maendeleo nchini.

CHADEMA kinapinga hatua ya Serikali ambayo viongozi na watendaji wake wakiwa wametajwa kama watuhumiwa katika habari zilizoandikwa na gazeti hilo imetumia mamlaka haramu ya Waziri mwenye dhamana ya sekta ya habari kugeuka mlalamikaji, mwendesha mashtaka na mfungaji huku ikipuuza taasisi za kusimamia uwajibikaji na haki.

CHADEMA ilitarajia badala ya kulifungia gazeti la MwanaHalisi ingewezesha kufanyika kwa uchunguzi huru kufuatia habari za kiuchunguzi zilizoandikwa na gazeti hilo juu ya watendaji na watumishi wa Serikali kuhusishwa na jaribio la mauji ya Dr Ulimboka Steven, kupanga njama za mauji ya viongozi wa CHADEMA na matukio mengine ambayo yenyewe ndiyo yenye mwelekeo wa kufanya wananchi wapoteze imani na vyombo vya dola hali ambayo inaweza kuhatarisha amani na mshikamano uliopo nchini.

CHADEMA kinalinganisha uamuzi huo wa Serikali uliotangazwa tarehe 30 Julai 2012 na Msajili wa Magazeti chini ya Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo kuwa ni sawa kujichukulia sheria mikononi kwa kuwa Serikali yenye kuheshimu misingi ya asili ya haki ingezingatia kwamba ikiwa chombo chochote cha habari kimedaiwa kuvunja sheria ama kukiuka maadili dhidi ya Serikali, viongozi wake ama watu binafsi mashtaka au malalamiko yangepelekwa kwa taasisi zinazohusika mathalani Baraza la Habari (MCT) au mahakama.

CHADEMA kinafahamu kuwa Serikali imeamua kulifungia kutochapishwa kwa muda usiojulikana gazeti la MwanaHalisi, kwa mujibu wa Sheria ya Magazeti ya mwaka 1976, kifungu Na. (25) (i); hata hivyo uamuzi huo ni kinyume cha misingi ya asili ya utawala wa sheria.

CHADEMA kinaelewa kwamba zipo sheria nyingine katika nchi yetu ambazo Serikali ingeweza kuzitumia kushughulikia madai iliyoyatoa kuwa Gazeti la Mwanahalisi limeandika habari na makala za uchochezi, uhasama na uzushi kupitia mahakama lakini imeamua kwa makusudi kuendelea kutumia sheria mbaya isiyokuwa na uhalali wa kihaki (illegitimate).

CHADEMA kinakumbusha kuwa kwamba Sheria hiyo ni kati ya Sheria zilizotajwa na Tume ya kukusanya maoni juu ya mfumo wa vyama vingi (Tume ya Nyalali) kuwa ni sheria mbaya miaka 20 iliyopita kuwa na Sheria mbaya na Serikali imekuwa ikikwepa kutunga sheria mpya pamoja na wadau wa habari kuandaa miswada ya sheria ya huduma za vyombo vya habari na uhuru wa taarifa kwa nyakati mbalimbali.

CHADEMA kinatoa mwito kwa wananchi na taasisi zote za kitaifa na kimataifa kufuatilia kwa karibu tukio hili la kufungiwa kwa gazeti la MwanaHalisi na matukio mengine ya hivi karibuni kuhusu asasi za kiraia, makundi mbalimbali katika jamii ikiwemo madaktari na vyama vya siasa hususan CHADEMA yenye kuashiria kwamba Serikali inayoongozwa na CCM imeanza mkakati wa kuficha ukweli na kudhibiti mabadiliko kwa kutumia sheria kandamizi, vyombo vya dola na njia nyingine haramu.

Hivyo, ieleweke kwamba hatua hii dhidi ya Gazeti la MwanaHalisi ni mwanzo tu wa hatua zingine zaidi dhidi ya magazeti mengine na taasisi nyingine hali ambayo inahitaji wananchi na wadau wote kuunganisha nguvu za pamoja katika kuchukua hatua za haraka kuinusuru nchi na mwelekeo huo.

Imetolewa tarehe 30 Julai 2012 na:

John Mnyika (Mb)
Mkurugenzi wa Habari na Uenezi

No comments: