Tuesday, July 31, 2012

Zitto Ahojiwa Kwa Rushwa

SAKATA la wabunge kuhusishwa na rushwa limeingia sura mpya, baada ya Naibu Kiongozi wa Upinzani Bungeni, Zitto Kabwe kuhojiwa na chama chake cha Chadema kwa saa tatu jana.
Wakati Zitto akihojiwa, kambi rasmi ya upinzani bungeni, iliwataja wabunge saba wa CCM na kueleza kuwa ndiyo wanaolichafua Bunge kwa kujihusisha na mambo yenye maslahi binafsi wakiwa watumishi wa umma.

Kadhalika, Naibu Spika wa Bunge, Job Ndugai alisema kwamba Taasisi ya Kuzuia na Kupamba na Rushwa (Takukuru) ilikuwa ikiendelea kuwahoji baadhi ya wabunge kuhusu tuhuma za rushwa na kwamba uchunguzi ukikamilika taarifa zitawekwa wazi.

Zitto ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Mashirika ya Umma (POAC) na Naibu Katibu Mkuu wa Chadema, jana aliandika katika ukurasa wake wa mtandao wa Tweeter kwamba alihojiwa na Sekretarieti ya chama chake kutokana na tuhuma za rushwa zinazowagusa badhi ya wabunge.
Katika maelezo yake, Zitto alisema aliiambia sekretarieti ya chama hicho kwamba Chadema kifanye uchunguzi ili kubaini ukweli wa suala hilo na kwamba yuko tayari kuwajibika ikiwa itathibitika kwamba alihusika kula rushwa.

“Kwa saa tatu nimejieleza mbele ya sekretariati ya chama kuhusu tuhuma za rushwa dhidi yangu. Niliomba kutaka kutoa maelezo kwa Katibu Mkuu, nimekiomba chama kufanya uchunguzi na ikibainika hatua zichukuliwe,” inasomeka sehemu ya taarifa hiyo kwenye Tweeter.

Lissu ataja wengine
Kwa upande wake, Mnadhimu Mkuu wa kambi hiyo, Tundu Lissu aliwataja wabunge wa CCM ambao wanatuhumiwa kuwa ni Nasir Abdallah (Korogwe Mjini), Mariam Kisangi (Viti Maalumu), Vicky Kamata (Viti Maalumu) na Charles Mwijage (Muleba Kaskazini) ambao hata hivyo, wote wamekanusha madai hayo.

Habari zaidi:  http://www.mwananchi.co.tz/habari

No comments: