Monday, July 16, 2012

Dlamini – Zuma ampiku Ping Addis Ababa

NKOSAZANA Dlamini-Zuma, kutoka Afrika Kusini, ameshinda uchaguzi mkali kuwa kiongozi mpya wa Tume ya Muungano wa Afrika. Bi Nkosazana Dlamini-Zuma, alimshinda kiongozi wa Tume hiyo anayeondoka Jean Ping wa Gabon, katika uchaguzi mkali uliopigwa mara kadhaa.

“hivi sasa tunaye kiongozi wa Tume ya Muungano wa Afrika Madam Zuma, ambaye sasa ataongoza siku za usoni za taasisi hii,” ndivyo alivyosema Rais wa Benin Thomas Boni Yayi ambaye pia ni mwenyekiti wa Muungano wa Afrika AU.

Dlamini-Zuma, mwenye umri wa miaka 63, ni balozi mwenye ujuzi na alikuwa mstari wa mbele katika kupigania uhuru nchini Afrika Kusini wakati wa Ubaguzi wa rangi. Yeye ni daktari wa mwanadamu na amewahi kuhudumu kama Waziri wa Afya, Maswala ya Nchini na waziri wa Mashauri ya nchi za Kigeni nchini Afrika Kusini.
Zuma ampongezab Dlamini

Mumewe wa zamani, ambaye pia ni kiongozi wa Afrika Kusini, Jacob Nzuma, alikuwa miongoni mwa watu wa kwanza kumpongeza kwa ushindi huo baada ya kura kupigwa katika mji mkuu wa Ethiopia, Addis Ababa.

Rais Zuma alisema; “Ushindi huu ni ufanisi mkubwa kwa Afrika, bara zima, umoja na mafanikio kwa wanawake ni muhimu sana.”

Ushindi wa Dlamini-Zuma umepatikana miezi sita tangu aanze juhudi za kumtimua mwenyekiti wa tume hiyo anayeondoka, Jean Ping. Katika mkutano kama huo kura ilipopigwa hakuna mmoja kati yao aliyepata thuluthi mbili ya kura kumwezesha kunyakua uongozi huo.

Iliamuliwa kuwa Ping aendelee kushikilia cheo hicho hadi usiku wa kuamkia leo aliposhindwa na Dlamini-Zuma. Rais Yoweri Museveni alishangilia kwa kusema: “huyu ni mpiganiaji Uhuru na si balozi wala kiongozi vivi hivi.”

Msemaji wa Ping, Noureddine Mezni, alisema Bwana Ping alimpongeza Madame Dlamini-Zuma na kumtakia kila la heri katika kazi yake mpya.

No comments: